31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

WANANCHI WANAHITAJI UMEME WA BEI NAFUU NA UHAKIKA

tanesco

KUMEKUWAPO na mjadala mzito juu ya uamuzi wa kupandishwa bei ya umeme hivi karibuni kulikotangazwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma ya Nishati na Maji (Ewura).

Ewura ilikubaliana na maombi ya Shirika la Ugavi wa Umeme nchini (Tanesco), ambalo liliwasilisha nia hiyo mapema Septemba mwaka jana.

Katika maombi hayo, Tanesco iliambatanisha sababu mbalimbali za kuwasilisha ombi hilo, ikizingatia gharama za uendeshaji, uzalishaji pamoja na kiwango kikubwa cha hasara wanachokipata kila mwezi ambacho ni Sh trilioni moja.

Tunakubaliana kuwa sababu zilizotolewa na Tanesco ni za kitaalamu. Tunakubaliana pia kukubaliwa ombi lao na Ewura ni la kitaalamu, ingawaje ilikubali kupanda gharama ya asilimia nane badala ya 18.1 waliyotaka waombaji.

Tunaona kwa msingi huo kuwa uamuzi wa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kuzuia matumizi ya gharama mpya za umeme ni za kitaalamu na kisiasa pia.

Aidha, uamuzi wa Rais Dk. John Magufuli kutengua uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Feleschi Mramba, ni wa kawaida na wa kisiasa kama njia mojawapo ya kushughulikia matatizo au masuala yoyote ya nchi.

Mamlaka ya uteuzi ndiyo ya utenguaji vile vile, hivyo uamuzi wa Rais ni halali kabisa.

Kimsingi tukiangalia uhalali wa kila sehemu yaani Ewura, Tanesco, Waziri wa Nishati na Madini na Rais Dk. Magufuli yatupasa kujiuliza swali moja; katika mtifuano huo wanapiganiwa wananchi ili tupate umeme wa gharama nafuu?

Hata hivyo, tunatakiwa kufikiri tofauti zaidi ya hapa. Tuhoji, tukosoe na kuwauliza wenye mamlaka wanapozungumzia umeme nafuu kwetu wananchi wa hali ya chini huwa wanamaanisha kitu gani?

Hebu tutafakari, tunapoambiwa umeme wa gharama nafuu sote tunafurahi na kuishia kwenye hoja hiyo tu, lakini hatuendelei kufikiri zaidi na kuangalia vigezo vya gharama nafuu ni nini!

Jambo la kwanza; kwa mfano umeme tuhoji umeme usio na uhakika, unakatika mara kwa mara na kuna uwezekano wa kuukosa kwa takribani saa 10 kwa siku!

Wengine wanakosa umeme kwa siku kadhaa katika miji mbalimbali, lakini ukifika; wakati wa utatuzi au gharama tunaambiwa ni umeme wa bei nafuu. Hiyo nafuu inaambatana na kukosekana ubora kwa maana ya kukosekana kwa uhakika wa umeme?

Umeme ambao unapatikana kwa zamu au mzunguko kwamba leo utawaka katika laini A, B, C na D; halafu wakazi wanaotegemea laini E, F, G, H, J, K, L na M wanaweza kukosa kwa takribani saa kadhaa au siku nzima si umeme wa maana.

Tunauliza hii ndiyo faida ya gharama nafuu au maana yake ni nini hasa?

Tuchukulie umeme huo unaotajwa kuwa nafuu, unakatika na kusababisha hasara ya vifaa vya kiwandani, vitu vya nyumbani na pengine nyumba kuungua. Huo ndiyo umeme wa bei nafuu?

Tunadhani Serikali yetu iko makini kwa sasa. Inataka umeme utakaotolewa uwe wa uhakika na bei nafuu kwa sababu hii inaendana na juhudi zake za Tanzania ya viwanda.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles