25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

WANANCHI WALALAMIKA AGIZO LA RAIS  KUPUUZWA

 

Na DERICK MILTON

WAKAZI wa Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu wamemlalamikia Mkuu wa Mkoa, Anthony Mtaka, kuwa wamekuwa wakiendelea kutozwa ushuru na halmashauri ya wilaya hiyo licha ya kupigwa marufuku na Rais John Magufuli.

Walikuwa wakizungumza katika mkutano wa hadhara  kwenye viwanja vya soko vya kata ya Dutwa.

Baadhi ya wananchi hao walimueleza RC Mtaka kuwa wamekuwa wakiendelea kutozwa wa Sh 200 kwa wauza mboga za majani, nyanya na matunda huku kwenye minada na magulio wakitozwa ushuru wa matandiko wa Sh 500.

Mmoja wa wananchi hao, Nhandi Masaka, alisema   rais alipiga marufuku halmashauri kuwatoza wananchi ushuru huo ambao ni kero.

“Tunafahamu na kutambua rais wetu alielekeza jambo hili… kila mara amekuwa akisema hataki kusikia au kuona wananchi wake hasa maskini wakitozwa ushuru wenye kero sasa mbona sisi tunatozwa?” alisema Masaka.

Naye Mariamu Dotto  alimtaka mkuu wa mkoa kuwafafanulia ukweli juu ya tamko la Rais Magufuli kama haliwahusu wao ikizingatiwa halmashauri kuendelea kutoza ushuru huo au wao wamekuwa wakielewa tofauti.

“Tunataka kujua hapa kwa nini halmashauri hii wanaendelea kututoza ushuru wa Sh 200 na Sh 500 sisi wajasiriamali, wauza mchicha, nyanya na matunda, au hatukulielewa agizo la rais wetu na kama tumelielewa kwa nini wanakaidi?” alihoji Mariamu.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu  Mtaka alisema agizo la Rais John Magufuli lilikuwa sahihi na ndivyo lilivyo.

Aliwashauri   wananchi kuacha mara moja kutoa fedha  ikiwa wataombwa kwa ajili ya ushuru huo.

“Kuanzia sasa ni marufuku mtumishi wa halmashauri kuja kwenye mnada, magulio kutoza ushuru wananchi wenye maisha ya chini, rais akisema hiyo ni sheria tayari na agizo,” alisema Mtaka.

Mtaka alisema   endapo mtumishi yeyote ataendelea kutoza ushuru huo, hatua kali dhidi yake zitachukuliwa,

Aliwataka wananchi kutoa taarifa kwake ikiwa wataombwa ushuru huo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles