23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

WANAFUNZI 22 WAFADHILIWA KUSOMA CHINA

Na LEONARD MANG’OHA -DAR ES SALAAM

NAIBU Waziri wa Nishati na Madini, Dk. Medard Kalemani, amekabidhi nyaraka za ufadhili wa masomo kwa wanafunzi 22 wanaotarajiwa kwenda nchini China kwa masomo ya juu katika kada za sheria, mafuta na gesi.

Akizungumza Dar e Salaam jana baada ya kukabidhi nyaraka hizo, Dk. Kalemani alisema hatua hiyo ni utekelezaji wa makubaliano ya miaka mitano baina ya Tanzania na China ya kutoa mafunzo katika nyanja hizo.

Alisema katika miaka mitatu ya kwanza ya makubaliano hayo, jumla ya wanafunzi 60 walikwenda nchini humo kwa masomo hivyo kuondoka kwa wanafunzi hao 22 watafanya idadi yao kufikia 82.

“Tunakwenda kusoma, twende na mtazamo wa kuja kudhibiti rasilimali zetu, kwa sababu si rahisi kudhibiti rasilimali kwa kusimamiwa na wageni.

“Tunakwenda kuwasomesha hawa waje kuwa wasimamizi wa rasilimali zetu, kwa mfano hawa wa sheria watatusaidia katika majadiliano ya mikataba ili rasilimali zisiibwe, isichotwe na kunyonywa,” alisema Dk. Kalemani.

Wanafunzi hao wanaotarajiwa kuanza masomo mwezi ujao, tisa ni wasichana na 13 ni wavulana, huku 10 wakiwa ni wa shahada ya pili na 12 ni wa shahada ya tatu (PhD).

Kalemani alisema wanafunzi hao watakaporudi watasaidia katika kuchoronga, kutafiti na kuchimba gesi na mafuta.

Aliwataka wanafunzi hao kuitangaza vema Tanzania na kuwa wazalendo kwa kuhakikisha wanarejea nchini baada ya kuhitimu masomo.

Mwakilishi wa Balozi wa China hapa nchini, Profesa Liu Yun, alisema uchambuzi wa kupata wanafunzi hao haukuwa mwepesi kutokana na idadi kubwa ya watu walioomba nafasi ila sifa za mwanafunzi mmoja mmoja ndicho kimetumiwa kama kigezo.

Mmoja wa wanafunzi hao, Nyamizi Twalib, aliziomba Serikali za Tanzania na China kuangalia uwezekano wa kuongeza muda wa makubaliano ili kutoa nafasi kwa vijana wengi kupata elimu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles