27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

WAMBURA AIKOMALIA TFF


Na CLARA ALPHONCE-DAR ES SALAAM   |

ALIYEKUWA makamu wa rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Michael Wambura, ameibuka na kusema hatakubali hadi kieleweke, baada ya Kamati ya Rufaa ya Maadili ya Shirikisho hilo kubariki adhabu ya kufungiwa maisha kujihusisha na soka.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Wambura alisema kuwa, hakubaliani na hukumu hiyo, kwa kuwa ipo kimkakati zaidi na imetoka katika mazingiza ya kimpira, lengo likiwa ni kumchafua aonekane na jamii yeye ni fisadi na mwizi.

Juzi Kamati ya Rufaa ya Maadili inayoongozwa na Wakili Ebenezer Mshana, ilitupilia mbali rufaa ya Wambura iliyokatwa mara tu baada ya Kamati ya Maadili kumfungia maisha kujihusisha na soka baada ya kukutwa na makosa matatu.

Kosa la kwanza ni kuchukua fedha za TFF, kwa malipo yasiyo halali, la pili ni kughushi barua ya kuelekeza alipwe na Kampuni ya Jack System Limited, huku akijua malipo hayo si halali, ikiwa ni kinyume cha ibara ya 73 (7) ya kanuni za maadili za TFF toleo 2013, na pia vitendo hivyo vimeshusha hadhi ya TFF, kinyume cha ibara ya 50 (1) ya Katiba ya TFF, kama ilivyoorodheshwa 2015.

“Kwanza napenda kusikitika sana na maamuzi yaliyofanyika juzi na Kamati ya Rufaa ya Maadili, kwani hukumu imekuwa ya kishabiki zaidi kuliko kisheria, nia ni kuwaambia wananchi kuwa mimi ni mbaya kiasi gani na mzuri kiasi gani.

“Maamuzi yote waliyozungumza mbele ya waandishi wa habari ni ya uongo, siyo tulioongea kwenye kikao, kesi nzima imekaa kimkakati, nadhani walijua labda mimi nina matumaini ya kushinda, toka mwanzo niliona dalili za kushindwa kwa sababu hata kupokea rufaa yangu walikuwa wanakimbia,” alisema Wambura.

Alisema kwa mujibu wa Ibara ya 74 (4) ya Madili ya TFF, Kamati ya Rufaa ya Maadili ni ya mwisho na hayatajadiliwa na chombo chochote.

Alisema lakini ibara ya 48 ya Mahakama ya Kimataifa ya Ushuluhishi ya Michezo (CAS), kwenda huko lazima uonyeshe kipengele cha sheria ambazo hujaridhika, ukiangalia sheria hizo na zile za nchi zinakinzana.

“Baada ya kupokea rufaa hiyo Jumatatu nitakaa na jopo la mawakili wangu kuona tutatumia njia ipi ambayo ni sahihi kwa ajili ya kupata haki, nimesikitishwa sana na wakili kusema uongo, hukumu nzima imejaa maneno mengi ya uongo na sina uhakika yaliyosemwa yatakuwapo kwenye hukumu,” alisema Wambura.

Wambura alisisitiza kuwa, nia yake ni kusafishwa na tuhuma hizo na kupata haki yake ambayo mpaka sasa anaona bado hajaipata.

- Advertisement -

Related Articles

1 COMMENT

  1. Kwa kweli mimi naona suala la kumfungia mtu katika masuala ya kisoka si sahihi kwa kuwa hayo mambo ni personal isues.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles