27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

WALIMA MPUNGA WASHAURIWA KUTUMIA MBEGU MPYA

Na Gurian Adolf-Sumbawanga


WAKULIMA wa mpunga wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa, wameshauriwa kutumia mbegu mpya ya mpunga aina ya SARO 5 TXD-306 ili wanufaike na zao hilo.

Hayo yalibainishwa na Ofisa Ufundi na Elimu wa Taasisi ya BRENT, Faustina Kalyalya anayetoa mafunzo ya kilimo bora cha mpunga kwa wakulima.

 

Akizungumza katika shamba darasa katika Kijiji cha Milepa wilayani humo, alisema taasisi hiyo ilianzishwa wilayani humo zaidi ya miaka mitano iliyopita ikiwa  na lengo la  kutoa elimu kwa wakulima katika suala zima la  kilimo bora sambamba na kuongeza  thamani katika mazao yao.

Alisema wakulima wa mpunga wilayani humo bado wanalima kilimo cha kizamani na kwa kutumia mbegu za kizamani bila kufuata  taratibu  za kilimo bora, hali ambayo inawasababisha kutopata tija  katika kilimo wanacholima.

Kalyalya alisema lengo kubwa la  kutoa elimu kwa wakulima hao ni kuona wanafanikiwa ambapo ni matarajio ya tasisi hiyo kuwa kila mkulima aweze kuvuna kwa kiwango cha gunia 40 za mpunga, hali ambayo itawawezesha kuona faida katika kilimo wanacholima.

Naye Ofisa Kilimo wa Wilaya ya Sumbawanga, Habona Kwileluya, alisema iwapo wakulima hao wakitumia mbegu ya mpunga aina  ya SARO 5 TXD-306 ambayo inaonekana kufanya vizuri katika bonde  hilo, watanufaika vizuri kwani asilimia kubwa ya wakazi wa bonde  hilo ni wakulima wa mahindi pamoja na mpunga.

 

Alisema ni vizuri wakulima wakafuata maelekezo ya wataalamu wa kilimo waliopo katika maeneo yao, ikiwa  ni pamoja na kulima  kwa wakati na matumizi ya pembejeo za kilimo tofauti na hivyo wasitegemee muujiza wa kupata mafanikio katika kilimo.

 

Mmoja wa wakulima anayepata mafunzo yanayotolewa na Taasisi ya Brent, Isaya Katepa, alisema tatizo lililopo hususani katika mafunzo kwa vitendo ni wakulima kutotaka kwenda kushiriki katika shughuli za mashamba darasa wakidai kuwa wao wanalima mashamba yao binafsi kwa hiyo hawana muda wa kwenda kulima katika mashamba darasa ambayo yameandaliwa kwa ajili ya mafunzo.

Katika msimu wa kilimo unaoisha hivi sasa, Brent imeanzisha mashamba darasa katika vijiji  vya Ng'ongo, Kaoze, Ilemba, Sakalilo na Milepa,

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles