PARIS, UFARANSA
RAUNDI ya kwanza ya uchaguzi wa rais wa nchini Ufaransa ilifanyika jana, ambapo Waziri wa zamani wa Uchumi Emmanuel Macron alikuwa akipewa nafasi kubwa kushinda.
Katika mfumo wa uchaguzi nchini hapa, rais huchaguliwa baada ya kufanyika duru mbili za uchaguzi.
Wagombea wakuu wanne wanawania wadhifa wa rais katika kinyang'anyiro kikali kutokana na wagombea kukaribiana.
Wakati Macron (39) akiwa mfuasi mkubwa wa Umoja wa Ulaya (EU) mpinzani wake wa chama cha siasa za mrengo mkali wa kulia, Marine Le Pen ni mpinzani mkubwa wa Umoja huo.
Le Pen pia anapigania kuiondoa sarafu ya Euro nchini Ufaransa na ameahidi kuitisha kura ya maoni ili watu wa Ufaransa waamua iwapo wanataka kujiondoa au kubakia EU kama Uingereza walivyofanya.
Hata hivyo, mashambulizi ya kigaidi nchini humo yanaonekana kumuongezea umaarufu Marine Le Pen.
Awali Macron alionekana kuwa na uwezekano wa kushinda katika duru ya kwanza kwa asilimia 24.5 ya kura, sasa amerudi nyuma kwa nusu pointi, wakati Marine Le Pen amepanda kwa pointi moja zaidi na kufikia asilimia 23.
Mgombea mwingine anayewakilisha siasa za kihafidhina Francois Fillon aliyewahi kuwa Waziri Mkuu wa Ufaransa pamoja na mgombea kutoka siasa za mrengo wa kushoto Jean-Luc Melanchon pia wamerudi nyuma kwa nusu pointi.
Mashambulio ya kigaidi yaliyotokea katikati ya mji mkuu, Paris yamekifanya kinyang'anyiro cha jana kisiweze kutabirika.