24.7 C
Dar es Salaam
Tuesday, March 19, 2024

Contact us: [email protected]

WADAU WAUNGE MKONO UTALII NYANDA ZA JUU


SEKTA ya Utalii nchini  ndiyo inayoongoza kwa kuliingizia taifa mapato ya kigeni baada ya kuipita sekta ya madini ikiwamo dhahabu.

Ni wazi hatua hiyo inatokana na mikakati mbalimbali iliyowekwa na serikali kupitia Shirika la Hifadhi ya Taifa (Tanapa) ambalo limekuwa likiendesha kampeni mbalimbali za kutangaza utalii   ndani na nje ya mipaka ya Tanzania.

Hivyo ni pamoja   na hifadhi na mapori ya akiba kadhaa ambayo rasilimali wanyama hujivinjari huku watalii kutoka mataifa ya nje nao wakifika kuangalia vivutia hivyo vya utalii.

Hivi karibuni,  Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Ally Hapi alitangaza kushirikiana na wakuu wenzake wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kutangaza fursa na vivutio vya utalii vinavyopatikana katika ukanda huo.

Hatua hiyo ni mwendelezo wa harakati za kuunga mkono azma ya Rais Dk. John Magufuli ya kufungua na kutangaza vivutio vya utalii vinavyopatikana katika ukanda wa Nyanda za Juu Kusini.

Ni wazi hatua hiyo ni moja ya mkakati wa RC Hapi, kuunga mkono jitihada zilizoanzishwa na mtangulizi wake aliyekuwa Mkuu wa Mkoa huo, Amina Masenza, za kuyaboresha  Maonyesho ya Utalii Karibu Kusini 2018 yanayoenda sambamba na maadhimisho ya Siku ya Utalii Duniani ambayo   yatafanyika mkoani Iringa Septemba 26 hadi 30 mwaka huu.

Tungependa  kuona watu kutoka maeneo mengine ya nchi   na hata nje wakishiriki kwa ukamilifu kwenye maonyesho hayo   waone na kutembelea vivutio vya utalii,  historia na kufahamu fursa za uwekezaji unaoweza kupatikana.

Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini inasifika kuwa na hifadhi zenye sifa za pekee ikiwamo Hifadhi ya Taifa ya Ruaha yenye makundi makubwa ya tembo na wanyama wengine.

Nyingine ni Hifadhi ya Kitulo yenye aina mbalimbali za maua ambayo hayapatikani mahali pengine duniani na Udzungwa yenye wanyama na viumbe adimu duniani kama vyura wa Kihansi.

RC Hapi kwa kushirikiana na wakuu wa mikoa wenzake wa Mbeya, Njombe, Songwe, Ruvuma, Rukwa na Katavi sasa wanakwenda kujipanga vema kwa kuwa na mkakati wa pamoja na kualika wadau  waunge mkono kwa dhati sekta ya utalii.

Si hilo tu hata   wananchi, taasisi na jumuiya mbalimbali ndani na nje kama zikijipanga vema kwa kushirikiana na sekta ya utalii ni wazi mkakati huo wa Mkoa wa Iringa na Nyanda za Juu Kusini utakuwa mfano mzuri wa kuigwa kwa   vitendo na kulinufaisha taifa katika maendeleo ya uchumi wake.

Mfano,   Mkoa wa Iringa mbali na vivutio vya hifadhi, pia una vivutio vya historia vinavyofahamika  kupitia Chifu Mkwawa ambaye alikuwa mstari wa mbele kwenye harakati za kupinga ukoloni hasa wa Wajerumani.

Tunatambua na kuthamini kila jambo jema linalofanywa na mtu mmoja mmoja, taasisi na hata kiongozi katika kuleta maendeleo.

Kwa maana hiyo ni wazi kazi inayofanywa  na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Ally Hapi ya kutekeleza  kaulimbiu ya kujenga uchumi imara kupitia sekta ya utalii ni muhimu iungwe mkono na wote wanaolitakia mema taifa hili na watu

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
584,000SubscribersSubscribe

Latest Articles