30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Wabunge wa CUF wapata ajali Dodoma

Na Khamis Mkotya, Dodoma

WABUNGE wawili wa Chama cha Wananchi (CUF) wamepata ajali walipokuwa wakisafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma kushiriki Bunge la bajeti linaloendelea.

Wabunge hao, Mbunge wa Wete, Mbarouk Salim Ally na Mbunge wa Viti Maalumu, Riziki Omar Juma, walipata ajali hiyo ajana asubuhi katika eneo la Mikese mkoani Morogoro, baada ya gari lao kupinduka.

Mbunge wa Ole, Mohamed Rajabu Mbarouk (CUF), alithibitisha wabunge hao kupata ajali na kueleza kuwa tayari mipango ya kwenda kuwachukua ilikuwa imefanywa.

“Ni kweli wabunge wetu wawili wamepata ajali leo (jana) asubuhi katika eneo la Bendera Mbili Mikese mkoani Morogoro. Walikuwa wanatoka Dar es Salaam kuja Dodoma.

“Tunashukuru wapo salama ingawa gari lao limeharibika limevutwa hadi Kituo cha Polisi, Mikese. Tumefanya mipango ya kwenda kuwachukua,” alisema na kuongeza:

“Pia tunashukuru Bunge kwani wametoa gari ambalo limekwenda Morogoro pamoja na wabunge wetu wawili wa wamekwenda huko,” alisema Mbarouk ambaye pia ni Waziri Kivuli (Sera, Uratibu na Bunge).

MTANZANIA ilimtafuta Mkurugenzi wa Bunge Habari, Elimu kwa Umma na Uhusiano wa Kimataifa, Jossey Mwakasyuka ambaye alisema hana taarifa zozote kuhusiana na ajali hiyo kwa sababu alikuwa nyumbani akiumwa.

Hata hivyo alimtaka mwandishi kufika ofisi ya Utawala na Rasilimali Watu, kwamba wao ndiyo wangeweza kuzungumzia suala la ofisi ya Bunge kutoa gari kwenda Morogoro.

Mwandishi alipofika katika ofisi hizo hakuweza kuonana na mkurugenzi wa idara hiyo baada ya kuelezwa kuwa alikuwa katika kikao na Spika Anne Makinda.

Mtanzania ilifanya mawasiliano na Mbunge wa Wete, Mbarouk Salim Ally ambaye alithibitisha kufuatwa na gari la Bunge.

“Kwa kweli hata sisi imetushangaza, hatukuweza kuelewa nini kimetokea tumekuja kushtuka tupo bondeni. Tulikuwa tunakwenda mwendo wa kawaida tu na mbele yetu kulikuwa na lori lakini kwa kweli hatujui nini kimetokea,” alisema. Mbarouk ameshinda uchaguzi wa ndani ya chama chake uliofanyika juzi.

Kwa mujibu wa Mbarouk, wabunge waliokuwa katika gari hilo la Bunge ambalo lilikwenda hadi Kituo cha Mikese kuwachukua walikuwa ni Mbunge wa Lindi Mjini, Salum Baruwani na Mbunge wa Mtambwe, Said Suleiman Said wote wa CUF.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles