27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

WAANDAMANA KUDAI LESENI ZA WANYAMA HAI

Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe
Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe

Na HUSSEIN OMAR-DAR ES SALAAM

JUMLA ya wafanyabiashara 100 wa Jijini Dar es Salaam, jana waliandamana ofisi ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, wakitaka kujua hatima ya leseni zao za kusafirisha viumbe hai nje ya nchi.

Akizungumza na MTANZANIA, Mwenyekiti wa wafanyabiashara hao Enock Balilemwa, alisema wamefikia hatua hiyo baada ya Serikali kushindwa kuwapa majibu ya msingi juu ya kusitishwa kwa leseni zao.

Alisema kilio chao kinatokana na zuio la Serikali kupitia wizara hiyo ambapo tangu Machi 17, mwaka huu wamewaingiza kwenye hasara ambayo kwa sasa hawawezi kuimudu.

“Januari mwaka huu tulilipa gharama zote na kufuata utaratibu juu ya kupata leseni au vibali hivyo lakini ghafla tulipata tangazo kutoka wizarani likitutaka kusitisha kusafirisha wanyama hao.

“Baada ya kuona tangazo hilo tuliandika barua mbili moja kwa katibu wa wizara hiyo na nyingine kwa Katibu Ofisi ya Rais kupitia kwa mwanasheria wetu ili kuomba kuonana na waziri mwenye dhamana lakini hatukupewa majibu ya kuridhisha.

“Mara nyingi kila tunapoomba kukutana na waziri ili atupe majibu ya kuridhisha imekuwa ni siasa tu na tuna taarifa kwamba leseni zetu zimefungiwa ili wapewe matajiri wa kizungu na kutunyang’anya sisi wazawa.

“Maisha yetu yamekuwa magumu kwani biashara zetu zimesimama hadi imefikia hatua taasisi za kibenki zinataka kuuza mali zetu ili kufidia mikopo tuliyokopa,” alisema.

Mwenyekiti huyo alisema leseni hizo ambazo waliomba na kusitishwa zina madaraja tofauti ambayo yanaruhusu kukamata wanyama hao.

“Daraja la 12 linaruhusu kukamata ndege, daraja la 13 linaruhusu kukamata tumbili la 15 linatupa kibali cha kukamata vyura,” alisema.

Mwenyekiti huyo alisema daraja jinigine ni la 16 ambalo linaruhusu kukamata mijusi na nyoka na daraja la 21 huwaruhusu kukamata wadudu.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Habari wa wizara hiyo, Doreen Makayo, baada ya kusikiliza madai ya wafanyabiashara hao aliwaahidi kuwasiliana na Waziri Maghembe ili kujua hatima yao.

“Baba zangu, wazazi wangu nimesikia kilio chenu ninawaahidi mara baada ya kikao hiki cha ghafla nitakwenda kuwapigia simu wahusika kisha nitawapa majibu yenu mapema iwezekanavyo,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles