27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Viwanja vya ndege vinavyoogopesha duniani

JOSEPH HIZA NA MASHIRIKA

KUSAFIRI kuelekea katika mapumziko mahali unapopahesabu kama paradiso ya kidunia ni ndoto ya wasafiri wengi waendao likizo.

Maeneo hayo paradise, ni yale yanayotajwa kuwa tulivu zaidi duniani, ambako ni tulizo tosha kwa kila mtu anayetaka kukaa mbali na kelele, michosho ya kazi au mjini.

Lakini kwa bahati mbaya, usipoangalia unaweza kubadili mawazo yako mara baada ya kushuhudia viwanja vya ndege katika baadhi ya maeneo haya tulivu zaidi duniani.

Mbaya zaidi utapatwa na kihoro, utakaposikia marubani wenyewe, watu ambao unawategemea kwa ujuzi wao, basi utue salama, lakini wanavilalamikia viwanja hivyo hatarishi.

Hiyo inatosha kukufanya upate woga wa kuwa na mpango wa kwenda kwenye mapumziko murua.

Tunaweza sema kwamba, hofu au woga wa kusafiri kwa ndege ni kitu cha kawaida kwa wasafiri wengi duniani.

Lakini pia, hata abiria wale wanaofahamika kwa ushupavu wao, wanaweza washindwe kutazama nje ya madirisha ya ndege wakati wakitua katika moja ya viwanja hivi vya ndege vyenye njia za kutua au kurukia zinazotisha zaidi duniani.

Kuanzia nchini Scotland hadi pande zile  za Antaktika, ni marubani wenye ujuzi na uzoefu tu wanaoweza kutua katika viwanja hivi.

Vinaweza kuwa katika maeneo hatari, pua na mdomo na milima au majabali au karibu mno na ufukwe wenye shughuli nyingi au kufikisha maji ya bahari kiwanjani hapo ama vyenye njia fupi mno.

Sababu ya viwanja hivi kutisha pengine ni kutokana na ukaribu wake na bahari, hivyo kuwa ngumu kupata eneo la kujenga njia zenye urefu wa kutosha kutua.

Hata kama ingekuwa ndani zaidi ya nchi kavu, njia ya kutua ndege inaweza kuwa hatari iwapo imejengwa karibu na eneo lenye shughuli nyingi za kibinadamu ikiwamo majengo na magari.

Au iliyozungukwa na milima na hata majabali hatari au yenye kukabiliwa na ukungu, maji ya baharini na barafu mara kwa mara.

Ukiachana na sababu za kijiolojia, utakuta viwanja vingine njia zao zimekatizwa na njia ya reli, ambazo gari moshi hupita humo mara kwa mara.

Miongoni mwa viwanja hivyo vinavyowapa shida na kuumiza vichwa marubani na hivyo kuwatisha wasafiri ni pamoja na Kiwanja cha Ndege cha Narsarsuaq huko Greenland.

Kingine ni Tenzing-Hillary nchini Nepal, ambacho hutumiwa zaidi na wapanda mlima Everest, ambacho njia yake imeishia futi 2,000 ikielekea bondeni.

Viwanja vingine ni Juanchoe Yrausquin huko Saba katika visiwa vya Caribbean, ambacho kinahesabiwa kuwa moja ya njia fupi zaidi duniani ikiwa na urefu wa futi 1,300 tu.

Kingine ni Lukla nchini Nepal, ambacho marubani hupata shida kutua, hivyo huwalazimu  kuzunguka muda mrefu ili kuitafuta njia huku uwanja wa Ndege wa Barra nchini Scotland marubani wakisubiri angani hadi mawimbi ya maji ya ufukweni yatakapoondoka.

Pichani ni miongoni mwa viwanja vinavyotisha wakati wa kutua.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles