Na Christina Gauluhanga, Dar es Salaam
Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (Veta), Chuo cha Kihonda, Morogoro kimebuni mfumo mpya wa kieletroniki wa kuongoza magari ambao utawasaidia askari kuepuka kugongwa mara kwa mara.
Akizungumza na Mtanzania Digital leo Julai 7, katika Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba (DITF), Mwalimu wa madereva wa magari makubwa kutoka VETA Kihonda, Wilium Munuo amesema mfumo huo humsaidia askari kuongoza magari akiwa pembeni ya barabara.
Amesema anachokifanya askari huyo ni kutumia mfumo huo kuruhusu magari yapite kwa utaratibu maalum.
“Mfumo huu ni Muhimu hapa nchini kwetu ambao umemebuniwa na wanafunzi pamoja na walimu kwakuwa askari huweza kuongoza taa akiwa amekaa pembeni,” amesema.
Amesema pia chuo hicho kinaendelea kuratibu shughuli mbalimbali ikiwamo ubunifu wa bidhaa nyingine ili wanafunzi waige.