33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

UTT AMIS ILIVYOSAIDIA KUBORESHA MAISHA YA JAMII

Mkurugenzi wa Masoko na Uhusiano wa UTT AMIS, Daud Mbaga (kushoto) akiwa na Mkurugenzi Mtendaji, ssa Wahichinenda.
Mkurugenzi wa Masoko na Uhusiano wa UTT AMIS, Daud Mbaga (kushoto) akiwa na Mkurugenzi Mtendaji, ssa Wahichinenda.

Na MWANDISHI WETU, Dar

WAKATI maelfu ya Watanzania wakinufaika na uwekezaji kwenye Kampuni ya Uwekezaji ya UTT AMIS, hatimaye taasisi za kimataifa zimeanza kutambua mchango wa kampuni hiyo kwa maendeleo ya uchumi na jamii kwa ujumla.

UTT, kampuni iliyo chini ya Wizara ya Fedha, kwa zaidi ya miaka 10 sasa imekuwa ikiwapa fursa Watanzania wenye vipato na nyadhifa tofauti kuwekeza kwa manufaa yao, watoto wao na taifa kwa ujumla.

Hatimaye, mwaka huu moja kati ya mifuko mitano ya UTT unaofahamika kwa jina la Mfuko wa Umoja (Umoja Fund), ulipiga hatua kubwa mbele pale ulipotunukiwa tuzo ya kimataifa ya CFI.co.

“Kwa sasa, UTT Asset Management and Investor Services Plc (UTT AMIS), ina mifuko mitano ya uwekezaji wa pamoja ambayo ni Mfuko wa Umoja; Mfuko wa Watoto; Mfuko wa Wekeza Maisha, Mfuko wa Jikimu na Mfuko wa Ukwasi,” anasema Mkurugenzi Mtendaji wa UTT AMIS, Dk. Hamis Kibola.

Katika miaka yake 10 ya utendaji, UTT AMIS ambaye ndiye MENEJA au msimamizi mkuu wa fedha zinazowekezwa na watu katika ‘miradi’ mbalimbali, inasimamia mtaji wa zaidi ya Sh bilioni 253, huku Mfuko wa Umoja ukiongoza kwa kuwa na uwekezaji mkubwa, ukiwa na zaidi ya Sh bilioni 213.

Ni kutokana na ukweli huo ndio maana haikuwashangaza wafuatiliaji wa masoko ua mitaji pale taasisi ya Capital Finance International (CFI) ilipoutuza Mfuko wa Umoja.

CFI ni miongoni mwa taasisi zinazoheshimika kimataifa zinazochapa na kusambaza habari, uchambuzi na maelezo ya kina (commentary) ya kiuchumi katika soko la habari duniani.

“Kwa kupitia tovuti yao pamoja na machapisho kadhaa, CFI huzungumzia kwa kina athari zinazosababishwa na masuala ya uchumi, siasa na biashara katika masoko.

“Kisha, machapisho hayo huja na mbinu za kutafuta suluhisho huku yakiyaweka hadharani maeneo na kampuni zenye mwelekeo wa kupata mafanikio,” anasema Dk. Kibola.

Kwa mujibu wa uchunguzi, machapisho ya CFI husomwa na zaidi ya watu 124,000 duniani kwa kila toleo, huku asilimia 33 ya machapisho hayo yakisambazwa barani Ulaya, asilimia 20 Amerika Kaskazini, 14 yakipelekwa Asia; asiliama 12 Mashariki ya Kati; asilimia nyingine 12 ni kwa ajili ya Amerika Kusini huku Afrika ikisambaziwa asilimia tisa ya machapisho hayo.

Kwa hakika taarifa na habari za kibiashara zinazochapwa na CFI hazibagua eneo lolote la dunia.

Kila mwaka, jarida hilo la mtandaoni huwasaka watu binafsi au taasisi zenye mchango wa kutukuka katika kukuza uchumi na kwa hakika kukuza na kuongeza thamani ya mitaji ya wana hisa husika, kisha kuwatuza kwa michango yao mahsusi.

“Kutokana na ukweli kwamba dunia ni kubwa na taasisi zinazofanya kazi ya kuwawezesha watu kuwekeza na kukuza uchumi ni nyingi, aghalabu shughuli za baadhi ya taasisi kama hizi hupita bila kutambulika,” inasomeka sehemu ya taarifa ya CFI.co.

Kwa kawaida, taasisi hupata nafasi ya kuwa moja kati ya washindani kutokana na michango inayopelekwa CFI na wasomaji au watu waliotembelea eneo husika.

Wapo wataalamu wakubwa wanaounda jopo la majaji ndani ya CFI na ni hao, bila ya upendeleo, hapendekeza taasisi zinazopaswa kushindanishwa.

“Ili kupata washindani, pamoja na vigezo kadhaa, CFI huzipitia taasisi husika na kuangalia mambo kadhaa kama vile namna yake ya kudhibiti matatizo (risk management), uwazi, ubunifu, ubora wa mawasiliano, utekelezaji wa uwekezaji na masuala mengine kadhaa,” inasema taarifa kutoka CFI.co.

 Walichonena majaji

UTT AMIS kupitia Mfuko wa Umoja, imepewa tuzo ya CFI.co, ikiwa ni miongoni mwa taasisi au kampuni kutoka sehemu mbalimbali duniani. Ifuatayo ni taarifa ya majaji wa taasisi hiyo kuhusu sababu ya kuitunuku UTT AMIS:

Tuzo ya Timu Bora ya Usimamizi wa Fedha Tanzania ya mwaka 2015.

Kataka kigezo cha wawekezaji wa kawaida na katika njia rahisi kabisa, UTT AMIS imeweza kusimamia kwa umakini mkubwa mifuko yake mitano yenye hisa katika miradi kadhaa iliyobinafsishwa.

UTT ya Tanzania ilibuniwa mwaka 2003 kwa ajili ya kukuza uwekezaji wa pamoja na kupigia debe utamaduni wa kuweka akiba.

Mfuko huu una hisa katika kampuni karibia zote zilizoorodheshwa, nyingi zikiwa ni zile awali zilizokuwa zikimilikiwa na serikali na baadaye kubinafsishwa katika miaka ya 1990.

Mwaka uliopita, UTT AMIS ilipewa ruhusu ya kufungua akaunti kwa wawekezaji kutoka mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kwa mujibu wa marekebisho ya sheria ya Capital Markets and Securities ya mwaka 2014.

Na sasa UTT AMIS ipo tayari kutoa huduma zake katika nchi za Kenya, Rwanda, Uganda na Burundi. Mifuko iliyo chini ya UTT-AMIS imewekezwa katika hisa na bondi zenye kutoa faida bila shaka yoyote.

Alama ya mifuko hiyo, Mfuko wa Umoja, ina miliki mali zenye thamni ya zaidi ya BILIONI 213, huku kukiwapo wawekezaji zaidi ya 121,000 ndani ya mifuko ya UTT AMIS. Pia Watanzania wanaoishi ughaibuni hukaribishwa kuwekeza.

UTT ni mrithi wa Mfuko wa Ubinafsishaji ulioanzishwa kwa ajili ya kutunza hisa kutoka katika kampuni zilizokuwa zikibinafsishwa na kuhakikisha ugawaji sawa wa hisa kwa Watanzania.

Jopo la majaji wa CFI.co linaichukulia UTT AMIS kama mfano wa kuigwa katika kukuza uchumi. Sera za wazi za UTT AMIS zimerahisisha na kuwapa nafasi wengi kuwekeza kwa kuondoa vikwazo bila kutetelesha ubora wa dhamana.

Na ndio maana majaji hatujasita kuwatuza UTT AMIS Tuzo ya Timu Bora ya Usimamizi wa Uwekezaji kutokana na tafiti zake nzuri kabisa zilizozaa matunda bora na kuifikia kisha kuiwezesha jamii.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles