24.4 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Utata kuhusu maumbile ya kike

MWANDISHI WETU

ASILIMI kubwa ya wanawake huwa hawafiki kileleni pindi wanapofanya mapenzi na wenza wao.

Hali hii imewafanya wengi kutopata raha kamili ya tendo la ndoa na hivyo kujikuta wakifanya tu mapenzi kwa lengo la kuwaridhisha wenza wao na wao kuishia njiani.

Wanaume wengi hawajui ni maeneo gani ya wanawake ambayo akishika ama kuchezewa anaweza kufikia kileleni, huu umekuwa ni mtihani mkubwa miongoni mwa wanaume na hata wanawake wenyewe.

Mwanahabari kutoka Marekani, Zoe Mendelson na aliyekuwa mpenzi wake mwaka 2016 waliwahi kubishana kuhusu suala la wanawake kufika kileleni na hawakuweza kupata jibu lililosahihi. Hali hiyo iliwafanya waingine katika mtandao wa Google na bado majibu waliyopata hayakuwaridhisha.

“Majibu yaliyokuja yalikuwa ya kipuuzi, takataka kabisa, nikaamua kuangalia katika majarida ya kitabibu,” Zoe aliliambia Shirika la Habari la BBC.

Anaongeza: “Lakini njia hiyo pia haikunisaidia, sikuelewa kitu. Sikujua ni viungo gani vya mwili walivyokuwa wakivizungumzia, mahali vilipo na kazi zake.”

Anasema aliona kuna tatizo kubwa kwani taarifa zote zilizopo mbele yake hazikuwa na maana ama hazikubaliki; pia akatambua kuwa hana chochote anachotambua kuhusu mwili wake.

Anasema miaka miwili baadae akiwa na rafiki yake María Conejo, ambaye ni mchora katuni kutoka nchini Mexico, waliamua kuanzisha mtandao unaoitwa Pussypedia: ensaiklopedia – kitabu kinachotoa taarifa kuhusu mambo mengi na ya kuaminika kuhusu mwili wa mwanamke.

Dhima kuu ya ukusanyaji wa taarifa hizo ulikuwa ni neno ‘pussy’, neon la Kingereza cha mtaani likiwa na maana ya sehemu za siri za mwanamke. Lakini watunzi wa ensaiklopedia hiyo wanalenga kulitumia kwa mapana zaidi, wakizungumzia mfumo mzima wa sehemu za siri za mwanamke. Akizungumzia kuhusu umuhimu wa kuanzishwa kwa mtandao huo Maria anasema: “Taarifa ni nguvu na aibu ni hatari. Nafikiri tunadharau maendeleo pale linapokuja suala la usawa wa kijinsi.” Anasema watu bado wanaishi katika dunia ambayo ina kiwango kikubwa cha kutokuwa na usawa na kuoneana aibu kuhusu miili yao na jinsia zao.

Anasema japo jamii inakuwa wazi zaidi, lakini bado wanaficha baadhi ya mambo.

María anasema: “Tunahisi kuwa tunajijua na kuijua miili yetu, ndiyo maana tunaona aibu kuuliza baadhi ya maswali. Tabia hii inatufanya tuwe na uelewa finyu.”

Zoe na María, kwa msaada wa wachangiaji wengine walianzisha Pussypedia Julai, mwaka huu.

Mtandao huo ambao unachapisha maudhui kwa lugha ya Kingereza na Kihispania, tayari umeshavutia wasomaji 130,000 tangu ulipoanza.

Wapo wanaouliza maswali kuhusu namna ya kusafisha sehemu za siri na iwapo dawa za kuua vijidudu zinaweza kusababisha ugumba.

MASWALI MAGUMU

Japokuwa Zoe na María wanafanya kazi kwa bidii kubwa kutafuta taarifa kutoka vyanzo vya kuaminika, baadhi ya maswali wanayokumbana nayo yamekuwa magumu kuyapatia majibu.

Hii ni kwa sababu uke – ukiachana na mfumo wa uzazi, umefanyiwa tafiti chache ukilinganisha na uume na kazi zake.

“Bado naendelea kutafuta majibu ya swali langu la awali,” anasema Zoe. “Kuna taarifa nyingi ambazo bado hazipatikani na kutokuwapo kwa makubaliano ya kisayansi juu ya fiziolojia ya mwanamke. Matahalani; hatujui hata ni tishu gani zilizopo katika kisimi zaidi.”

“Ukitafuta neno uume katika jarida lolote la kitabibu ama kitabu cha afya, utapata majibu mengi na yenye kueleweka. Lakini hali huwa ni tofauti unapotafuta neno uke,” anasema Zoe.

Japo María anaeleza kuwa uwapo wa taarifa kwa wingi haumaanishi kwamba ufahamu mkubwa.

“Nafikiri hata wanaume wanajua haya kwa kiasi kidogo mno. Japo kuna wingi wa taarifa, kuna tabia ya wanaume kujiona wapo juu na wanajua kila kitu, hali inayowafanya wengi wao kutojua mengi kuhusu miili yao na kidogo zaidi kuhusu miili yetu,” anasema Maria.

Wanawake wana kiu zaidi ya kujua. Kiasi kwamba, pale María na Zoe walipoanzisha kampeni yao ya kukusanya fedha kwa ajili ya kuanzisha Pussypedia, walipita lengo walilolijiwekea ndani ya siku tatu, na kujikuta wakikusanya Dola za marekani 22,000 – mara tatu zaidi ya lengo lao la awali.

Fedha hizo ziliwaasaidia María na Zoe kuanza, lakini hiyo ni baada ya miaka miwili ya kufanya kazi bure. Sasa hivi wanahitaji kutengeneza fedha kutoka Pussypedia ili waweze kuwalipa wachangiaji kwa maudhui yao na kufanya mtandao huo kuwa sawa muda wote.

Mtandao huo huwapa fursa wasomaji kuchangia chochote, pia huuza bidhaa kupitia michoro ya María.

“Nimejaribu kuuchora mwili wa mwanamke kwa miaka mitano, katika namna ambayo nitautendea haki.

“Nataka kuonesha mwili wa mwanamke anayeustadi mwili wake. Nataka kubadili fikra juu ya mwili ulio wazi jinsi unavyoonekana. Pussypedia imeniwezesha kufanya yote niliyojifunza kwa ustadi,” anasema Maria.

Zoe pia anataka kutanua wigo na kuweka maudhui kuhusu watu wanaobadili jinsi na afya yao, eneo ambalo hadi sasa hawajaliwekea kitu.

Lakini pia, anaamini katika siku za hivi karibuni atapata majibu na kuweka maudhui juu ya swali lake la msingi, kuhusu iwapo wanawake wote hufika kileleni.

MTANDAO UNAOSAIDIA WASICHANA KUBAINI IWAPO UKE WAO NI WA KAWAIDA

Nchini Uingereza, wasichana huhimizwa kutumia huduma ya mtandaoni ili kuwasaidia kuangalia iwapo maumbile ya uke wao ni ya kawaida.

Huduma hiyo hupatikana katika mtandao wa masuala ya afya ya uzazi na ngono wa Brook, unaotoa mifano kwa kutumia video na kutoa ushauri kuhusu jinsi sehemu za siri za mwanamke zinavyobadilika wakati wa kubalehe au kuvunja ungo.

Lengo kuu ni kuwahamasisha wasichana kujikubali walivyo.

Watafiti wa afya waliotengeneza mtandao huo wanasema wana matumaini kwamba wasichana wataanza kujiamini zaidi na kuwafanya kutotamani kufanyiwa upasuaji wa kubadili mwonekano wa sehemu zao siri.

Hii ni kwa sababu wasichana wengi nchini humo hupenda kufanyiwa upasuaji ili kubadili maumbile yao wanayodhani kwamba hayajakaa katika mwonekano wa kawaida kama walivyo wengine.

Wengi wanaofanya hivyo ni wale wenye umri chini ya miaka 18.

Upasuaji huo wa urembo wa sehemu nyeti maarufu ‘labiaplasty’  hufanywa kwa lengo la kuongeza au kupunguza sehemu hizo.

Upasuaji huo hutekelezwa na madaktari binafsi ambao hutoza maelfu ya mapauni.

Mara nyingi hufanywa na mamlaka ya huduma ya afya – NHS iwapo sehemu nyeti za msichana zina kasoro na zinamsumbua au zinamwathiri kiafya.

Madaktari wa afya hawatakiwi kuamua kumfanyia msichana upasuaji kwa sababu ya urembo pekee.

Kulingana na takwimu za NHS, zilizotolewa mwaka 2015/16, zaidi ya wasichana 200 walio na umri chini ya miaka 18 walifanyiwa upasuaji wa sehemu zao za siri na zaidi ya 150 ya wasichana hao walikuwa chini ya miaka 15.

Louise Williams, ni muuguzi katika chuo kikuu cha College Hospital na kiongozi wa mradi huu, anasema: “Elimu hii itawasaidia wasichana kuelewa sehemu zao za siri na jinsi inavyokomaa wakati wanapovunja ungo, hasa wakiwa na wasiwasi jinsi wanavyojitizama au kijihisi.

“Sehemu za siri za wasichana huwa zina maumbo tofauti na ukubwa fulani, kwa hiyo si jambo la ajabu kuwa tofauti na mwingine,” anasema.

Dk. Naomi Crouch, kutoka chuo cha taasisi cha Royal College cha Madaktari wa uzazi na wataalamu wa afya ya uzazi na Shirika la Uingereza la Watoto ambao pia walihusika katika utafiti huo anasema: “Hakuna utafiti wowote wa kisayansi unaounga mkono upasuaji wa sehemu za siri na iwapo una athari zozote za kimwili au kisaikolojia hasa kwa vijana ambao bado wanakua.

“Tunatumai kwamba ujumbe huu utawapatia wasichana ufahamu zaidi kwamba, sehemu zao za siri ni maalumu na hubadilika wanapokua maishani na ni kawaida.”

MADHARA KUBADILI UKE

Yapo madhara mengi yanayoweza kujitokeza mtu anapobadili uke wake. Miongoni mwa madhara hayo ni uvujaji wa damu, kupata maambukizi, uharibifu wa tishu za mwili na kupunguza hisia za sehemu za siri.

Madhara mengine ni kuganda kwa damu katika mishipa na kuathirika na dawa za kulala pindi unapofanyiwa upasuaji.

Upasuaji huo huhusisha kupunguzwa au kubadilishwa umbo kwa midomo ya uke wao.

KISA CHA ANNA

Anna (si jina lake halisi), alitaka kufanyiwa upasuaji wa labiaplasty akiwa na umri wa miaka 14.

“Nilipata wazo la kufanyiwa upasuaji kutoka kwa watu wengine, niliona kama uke wangu haukuwa umekaa vyema vya kutosha au haukuwa wa kupendeza hivyo nilitaka upunguzwe.

“Niliona tofauti kati ya uke wangi wa watu wengine baada ya kuangalia video za ngono, nikapata wazo kwamba uke unafaa kuwa umelainika na hautakiwi kuwa na kitu kinachojitokeza nje.

“Nilidhani hivyo ndivyo ambavyo kila mtu anatakiwa kuwa, kwa sababu sikuwa nimeona picha za watu wa kawaida kabla ya hapo.

“Nakona ni vema niofanyiwe upasuaji ili niwe sawa na wengine, lakini baadaye nilibadili msimamo wangu na kuamua kutofanyiwa upasuaji.

“Sasa hivi, nafurahi kuona kwamba sikufanyiwa upasuaji. Siuhitaji. Uke wangu ni wa kawaida kwa asilimia 100,” anasema.

Paquita de Zulueta, ni daktari wa kawaida aliyefanya kazi kwa zaidi ya miaka 30, anasema ni miaka ya karibuni tu ambapo wasichana wameanza kwenda kwake wakilalamika kuhusu mwonekano wa uke wao.

“Nawaona wasichana wa miaka 11, 12, 13 ambao wanafikiria uke wao una tatizo – kwamba labda una umbo lisilo sahihi, ni mnene au mdogo sana, na wanakerwa na hali hiyo.

“Wengi wanaamini kwamba midomo ya ndani ya uke wao haifai kuonekana, wanadhani uke unafaa kuwa kama mwanasesere au Barbie hivi, lakini uhalisia ni kwamba kuna tofauti kubwa katika mwonekano wa uke wa wanawake. Ni kawaida kwa midomo ya ndani kujitokeza nje,” anasema daktari huyo.

Analaumu picha ambazo si za uhalisia ambazo wasichana wengi wanakutana nazo kupitia video na picha chafu za ngono na pia katika mitandao ya kijamii.

“Wasichana wanapaswa kuelimishwa kuhusu sehemu zao za siri tangu wakiwa wadogo, kuwaeleza kwamba kuna tofauti kubwa katika uke wa wanawake mbalimbali – yaani kama tulivyo tofauti usoni ndivyo tunavyotofautiana hata katika sehemu nyeti,” anasema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles