MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam imeahirisha kesi ya msanii wa filamu maarufu nchini, Wema Sepetu hadi Machi 15, mwaka huu kutokana na upelelezi kutokamilika.
Wema ambaye ni Miss Tanzania 2006, anakabiliwa na kosa la kukutwa na bangi katika upekuzi uliofanywa na polisi nyumbani kwake Februari 4, mwaka huu maeneo ya Ununio jijini Dar es Salaam.
Kesi hiyo ilikuja leo kwa ajili ya kutajwa ambapo Wakili wa Serikali Nasoro Katuga alidai upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika hivyo Hakimu Mkazi Thomas Simba aliahirisha shauri hilo hadi Machi 15.
Msanii huyo alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Februari 9, mwaka huu ambapo aliachiwa baada ya kupata dhamana ya Sh milioni tano.