Kulwa Mzee, Dar es Salaam
Mfanyabiashara Hariri Mohammed Hariri, anayekabiliwa na tuhuma za kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroin anaendelea kusota rumande kwa zaidi ya miezi tisa kutokana na upelelezi wa shauri hilo kutokamilika.
Hayo yamebainika leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakati kesi hiyo ilipokuwa inatajwa mbele ya Hakimu Mkazi Janeth Mtega.
Wakili wa Serikali, Esther Martine, alidai mahakamani kwamba upelelezi haujakamilika hivyo aliomba tarehe nyingine ya kutajwa.
Mahakama iliahirisha kesi hiyo hadi Desemba 12, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa, mshtakiwa alirudishwa rumande.
Hariri alifikishwa mahakamani akidaiwa kutenda kosa hilo, Machi 2, mwaka huu, maeneo ya Kinondoni Matitu, Dar es Salaam.
Mshtakiwa anadaiwa siku hiyo alikutwa akisafirisha gramu 214.11 za dawa za kulevya aina ya heroin.