33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

UNAWEZA KUACHA SIGARA KWA KUTUMIA DAWA ZENYE NICOTINE

TUMBAKU ni moja ya mimea ambayo hapa nchini na katika mataifa mengine duniani, hutumika kama zao la biashara linaloongeza kipato.

Zao hili hutumika kutengeneza sigara ambazo zimekuwa zikitumika kama kiburudisho kwa baadhi ya watu.

Uwezo wa tumbaku kutumika kama kiburudisho kwa baadhi ya watu, inatokana na mmea huu kuwa na kemikali ya asili ambayo hujulikana kwa jina la ‘nicotine.’

Pamoja na kutumika kama kiburudisho kwa baadhi ya watu, tumbaku imekuwa na athari za kiafya ambazo zimesababisha kuwa na utaratibu wa matibabu yanayojumuisha matumizi ya kemikali inayopatikana katika tumbaku (nicotine).

Baada ya kutumika, husababisha mabadiliko kadhaa kutokea mwilini, mfano; kuzalishwa kwa homoni (epinephrine) ambayo huifanya mishipa ya damu kusinyaa (constrictions of Arteries), moyo kushindwa kusukuma damu ili iweze kufika katika viungo vingine vya mwili na  mapigo ya moyo kuongezeka.

Pia kemikali hii, husababisha vidonda vya tumbo ambavyo huchelewa kupona.

Pamoja na athari tajwa za kiafya, baada ya kutumia nicotine, pia matumizi yake yamechangia utegemezi kwa mtumiaji (Nicotine Addiction). Hali hii ya utegemezi imesababisha ugumu kwa baadhi ya watumiaji kushindwa kuacha uvutaji wa sigara au bidhaa zenye nicotine.

Kwa huduma au matumizi ambayo ni ya kitabibu, imekuwa ikitumika kama sehemu ya kumsaidia mtumiaji wa tumbaku au sigara kuweza kuacha matumizi hayo (Recreational drug).

Kuna dawa ambazo zimeandaliwa kwa kutumia nicotine ili kumsaidia mtumiaji wa tumbaku kuacha matumizi hayo, ambazo ni zile zinazotumika kwa njia ya kupuliza (nasal spray), kutafuna (nicotine gum), vidonge na kuvuta (inhaler).

Dawa hizi humsaidia mtumiaji wa sigara au bidhaa zenye nicotine kuacha kabisa. Kama ilivyo kwa dawa nyingine zinazotumika katika matibabu, huwa kuna muingiliano (interactions) wa dawa za aina tofauti pindi zinapotumika kwa pamoja katika mwili wa mtumiaji. Muingiliano huo unaweza ukawa ni wenye manufaa kwa mtumiaji au ni wenye kuleta madhara.

Miongoni mwa dawa ambazo zinamuingiliano na bidhaa za tumbaku katika matumizi ni pamoja na dawa zifuatazo:

Zinazotibu matatizo ya moyo au shinikizo la damu (Propranolol), dawa za kisukari (Insulin), hii inatokana na nicotine kuwa na uwezo wa kuathiri namna ambavyo mwili unatawala kiwango cha sukari mwilini, hususani katika uwezo wa insulin kufanya kazi.

Dawa nyingine ambazo zinamuingiliano na nicotine ni za pumu, ambazo uwezo wake unapungua endapo zitatumika sambamba na nicotine.

Pia dawa za kutibu vidonda vya tumbo zitashindwa kufanya kazi kwa kiwango kinachohitajika kutokana na kemikali hii yenyewe kuwa na uwezo wa kumsababishia mtu apatwe na matatizo ya vidonda vya tumbo.

Pamoja na muingiliano huo wa nicotine na baadhi ya dawa, kemikali hii imekuwa ikisababisha kupunguza hamu ya kula. Sababu hii imekuwa ikituiwa na baadhi ya watumiaji katika kutatua changamoto ya uzito mkubwa. Mtumiaji anatumia nicotine gum na bidhaa nyingine zenye kemikali hii katika kupunguza uzito wa mwili wake.

Kwa matumizi ambayo ni tahadhari kwa bidhaa, jamii ya tumbaku, haishauriwi nicotine kutumika kwa mjamzito.

Tafiti zinaonyesha kuwa kina mama ambao ni watumiaji wa bidhaa zenye nicotine wamekuwa wakijifungua watoto  wenye matatizo katika baadhi ya viungo/maumbile ya miili yao.

Pamoja na tumbaku kuwa na kemikali aina ya nicotine, ambayo imekuwa ikitumika katika mifumo mbalimbali ya matibabu, ni vyema kuzingatia faida na hasara za kemikali hii kabla ya kufanya matumizi yake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles