23.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

UFARANSA KUISAIDIA TANZANIA KUFIKIA MALENGO


Na MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM

Ufaransa  imeelezea utayari wake kushirikiana na Tanzania na kuhakikisha lengo la nchi kuwa na uchumi wa kati kufikia mwaka 2025 linafikiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana wakati wa ziara ya wabunge watatu wa bunge la nchi hiyo hapa nchini, Balozi wa Ufaransa hapa nchini, Frederic Clavier, alisema nchi yake itaendelea kusaidia jitihada za maendeleo.

Balozi Clavier alisema nchi yake kupitia Shirika lake la Maendeleo (AFD),  itaongeza  kiwango inachotoa kusaidia maendeleo kufikia Euro milioni 100 kutoka Euro milioni 50  za sasa na hivyo kusaidia kasi ya Serikali kuwaletea wananchi wake maendeleo.

“Kiasi hiki cha pesa kitakachotolewa kitasaidia kugharamia miradi ya maji, miundombinu pamoja na nishati. Ufaransa pia ipo tayari kufadhili miradi mingine ya maendeleo kadiri Serikali ya Tanzania itakavyoiainisha na kuileta,” alisema.

Kwa upande wake mkuu wa ujumbe huo wa wabunge watatu, Ronan Dantc, alisema Serikali ya nchi yake inaichukulia Tanzania kama mdau kutokana na kuwa na fursa nyingi za kiuchumi na kibiashara ambazo zina manufaa kwa pande zote mbili.

“Mimi si mara yangu ya kwanza kufika Tanzania na naifahamu vyema Tanzania kama nchi nzuri yenye amani, watu wakarimu na rasilimali nyingi. Ufaransa inaiona Tanzania kuwa ni mdau muhimu kwa maendeleo na ipo tayari kuunga mkono jitihada za kuleta maendeleo kwa watu wake,” alisema.

Mbunge huyo alisema katika ziara yao hiyo ya kikazi wamepata fursa ya kutembelea sehemu mbalimbali na wameona fursa nyingi katika maeneo mbalimbali ikiwamo katika sekta ya utalii ambayo alisema inaweza kuendelezwa zaidi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles