23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Trump azidi kuwekwa mtu kati sakata la Ukraine

WASHINGTON, MAREKANI

SI jambo la kawaida unaposhuhudia rais akiwa katika hatari ya kutimuliwa madarakani na bunge. 

Rais wa Marekani anaweza kuvuliwa madaraka endapo ”atakiuka sheria”. 

Sheria zinazosimamia kuvuliwa madaraka kwa rais sio rahisi na wachambuzi wa mambo hawana imani iwapo azimio la Democrats kumng’oa madarakani Rais wa Marekani, Donald Trump litafaulu.

Wakati kukuwa na sintofahamu hiyo, Balozi wa zamani wa Marekani nchini Ukraine Marie Yovanovitch ametoa ushahidi kuhusu kuondolewa kwake ghafla katika wadhifa wake wakati wa siku ya pili ya kusikilizwa hadharani ushahidi unaoweza kusababisha kufunguliwa mashtaka na kuondolewa madarakani kwa Rais Trump.

Wakati wa ushahidi wake mbele ya Kamati ya Bunge ya Ujasusi, Trump alikuwa kwenye mtandao wa Twitter akimshambulia mwanadiplomasia huyo na rekodi yake.

Aliandika kuwa kila mahali alikofanya kazi Marie Yovanovitch mambo yalikwenda mrama. 

Mwenyekiti wa kamati hiyo ya Bunge kutoka chama cha Democrat, Adam Schiff aliisoma kauli hiyo ya Trump kwa Yovanovitch wakati wa kikao hicho, akimuuliza jibu lake.

“Siwezi kuzungumzia kile rais anajaribu kukifanya, lakini nadhani athari ni kutisha,” alisema. 

Ujumbe huo wa Twitter ulizusha shutuma za haraka, huku wanachama wa Democrat  wakisema kilikuwa kitendo cha kuwatisha mashahidi.

Yovanovitch anayefahamika kwa rekodi yake ya kupambana na rushwa, alipelekwa Ukraine 2016 ambako alihudumu kama balozi wa Marekani hadi alipolazimika kuondoka Mei 2019.

Schiff alisema kuondolewa kwake kulisaidia kuweka mazingira ya kufunguliwa njia isiyo rasmi, ya kuendesha sera ya Ukraine ambayo ilitumiwa na Trump na washirika wake kuishinikiza Ukraine kuwachunguza wapinzani wa kisiasa wa rais huyo.

Yovanovitch anaungana na maafisa wengine kutoa ushahidi kwenye mchakato wa kihistoria ambao wanachama wa Democratic wanautegemea kupata hoja za kumfungulia mashtaka yanayoweza kumuondoa madarakani rais Trump.

Wapinzani wa Democrats wanasema Ikulu ya White house ya Trump imefikia katika kile walichokiita “kiwango cha kabuli jipya lisilokuwa na sheria”

Si jambo la kawaida unashuhudia rais akiwa katika hatari ya kutimuliwa madarakani na bunge.

Uchunguzi huu ni aina ya mahojiano ya kesi ambayo yanaweza kusababisha kung’olewa madarakani kwa rais na bunge la Congress.

Baadhi ya watu wanafikiria kuwa uchunguzi huu ni hatua halisi ya kumg’oa madarakani rais wa nchi , lakini ukweli ni kwamba ni mwanzo tu wa mchakato wa hatua mbili ambazo hufanyika katika mabunge mawili ya Marekani.

Kwanza wabunge katika Baraza la wawakilishi huangalia ushahidi na kuamua ikiwa wanataka kushinikiza mashtaka dhidi ya rais – au kama kama inavyoelezwa ”kupendekeza kufanyiwa uchunguzi wa tuhuma “.

Lakini ni Bunge la juu zaidi, ama Seneti, lenye mamlaka ya kuendesha kesi, ikiwa rais atapatikana na hatia, halafu yeye anaondolewa madarakani makamu wa rais huapishwa.

Ni marasi wawili tu wa Marekani ambao wamewahi kushtakiwa, Andrew Johnson mwaka 1868 na Bill Clinton mwaka 1998. 

Wote walichunguzwa katika bunge lakini baadaye Seneti ikawaondolea hatia.

Mwaka 1974, Rais Richard Nixon alipatikana akiwa anawafanyia ujasusi wapinzani wake katika sakata linalofahamika kama Watergate – alijiuzulu kwasababu alijua kuwa atahojiwa mbele ya Bunge na kung’olewa madarakani na Senati

Trump anashutumiwa kutumia vibaya mamlaka aliyonayo na kufanya mchezo mchafu ili kuongeza nafasi yake ya kuchaguliwa tena mwaka ujao.

Trump anashutumiwa kuacha kutoa usaidizi wa kijeshi kwa Ukraine ili kuilazimisha nchi hiyo imchunguze hasimu wake kisiasa, Joe Biden

Anadaiwa kumshinikiza rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, kuchunguza taarifa zinazoichafulia jina familia ya Joe Biden – aliyekuwa Makamu wa rais wa Barack Obama ambaye naaminiwa kuwa anaweza kuwa mshindani mkuu wa Trump katika kinyang’anyiro cha kuingia ikulu ya White House 2020.

TRUMP ALIVUNJA SHERIA?

Trump anasema hakufanya kosa lolote na ameuita uchunguzi huu dhidi yake mchakato “dhaifu, ulijaa udanganyifu, wa kuvuruga mambo na wenye upendeleo wa hali ya juu “. 

Ikulu ya White House inasema kuwa haitafanya ushirikiano wowote katika uchunguzi huu.

Lakini amekuwa katika kipindi kigumu tangu mfichuaji wa sakata hii alipolalamika juu ya simu aliyompigia rais wa Ukraine Zelensky Julai 25.

Trump alikuwa amezuia mamilioni ya dola ya msaada wa kijeshi wa Marekani kwa Ukraine na maafisa wa ngazi ya juu wamesema kuwa aliweka wazi kwamba hatatoa pesa hadi pale Ukraine itakapoanza uchunguzi dhidi ya hasimu wake ingawa Ikulu ya Marekani inakanusha hili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles