24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

TRUMP AONYA MATAIFA KUFANYA BIASHARA NA IRAN

NEW YORK, MAREKANI


RAIS Donald Trump, jana ameyaonya mataifa kutothubutu kufanya biashara na Iran, huku akisifu vikwazo vipya dhidi ya taifa hilo kuwa vikali zaidi kuwahi kuwekwa, hatua iliyoibua mchanganyiko wa ghadhabu, hofu na uasi nchini humo.

Kupitia ukurasa wake wa twitter, Trump aliandika kuwa vikwazo dhidi ya Iran tayari vimeshawekwa.

“Hivi ni vikwazo vikali zaidi kuwahi kuwekwa, na Novemba tutangaza vikwazo vingine,” aliongeza Trump.

Aliongeza kuwa yeyote anayefanya biashara na Iran, hatafanya biashara na Marekani, na kwamba anachokitafuta ni amani duniani, na si zaidi ya hapo.

Muda mfupi tangu kuanza kutekelezwa kwa vikwazo hivyo, kampuni ya magari ya Ujerumani ya Daimler, ilitangaza kusimamisha biashara zake nchini Iran.

Taarifa ya Daimler ilisema wamesitisha shughuli nchini humo kutokana na vikwazo hivyo vilivyoanza kutekelezwa, na kuongeza itaendelea kufuatilia kwa karibu hatua za kisiasa.

Wairan wengi, ikiwa ni pamoja na wafanyabiashara wa magari, wanailaumu Serikali yao kwa kurejeshwa vikwazo hivyo vya Marekani, lakini pia wanahofia huenda vikawa ni pigo la mwisho kwenye uchumi wa taifa hilo unaoyumba.

Kujiondoa kwa Trump kwenye mkataba wa nyuklia wa mwaka 2015, Mei mwaka huu, tayari kuliwaogopesha wawekezaji na kuchochea kushuka kwa thamani ya sarafu ya Iran – riali, kabla hata ya vikwazo hivyo kuanza kutekelezwa upya.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Mohammad Javad Zarif, amewaambia wanahabari kuwa namna ambavyo dunia imeijibu hatua hiyo ya Trump, imeonyesha kutengwa kwa Marekani kidiplomasia.

Mmoja wa wafanyakazi wa sekta ya ujenzi, alisema akiwa katika mtaa mmoja mjini Tehran, anajisikia kama maisha yake yamevurugika.

Alisema vikwazo hivyo tayari vimekwishaathiri kwa kiasi kikubwa maisha ya watu, na kwamba hawezi hata kununua chakula, wala kulipa kodi ya nyumba.

Serikali za Ulaya zimeeleza kughadhabishwa na mkakati huo wa Trump, unaosababisha biashara zao zilizopo Iran kukabiliwa na kitisho cha kuadhibiwa kisheria na Marekani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles