30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

TRUMP ANACHOCHEA MATUMIZI YA SILAHA ZA NYUKLIA

trump-putin-large_trans_nvbqzqnjv4bqeo_i_u9apj8ruoebjoaht0k9u7hhrjvuo-zlengruma

Na MARKUS MPANGALA- DAR ES SALAAM

HAIJAWAHI kutokea kiongozi wa nchi yeyote akatamka hadharani kuwa nchi yake inahitajika kuongeza kasi ya kumiliki silaha za nyuklia. Haijapata kutokea au kuonekana rais wa nchi anasisitiza matumizi ya silaha za nyuklia ambazo zimesababisha mgawanyiko mkubwa baina ya mataifa makubwa dhidi ya madogo kiuchumi.

Swali kubwa linaloulizwa ni nani anastahili kumiliki silaha za nyuklia na nani hastahili? Na je, kama kumekuwa na uhalali wa kumiliki silaha za nyuklia kwa mataifa makubwa ya kiuchumi kama Marekani, Urusi, India, Pakistan, Afrika Kusini, Japan, Korea Kaskazini na Kusini, Uingereza, Ufaransa kwa kuzitaja chache. Nchi hizo zimekuwa kwenye mahangaiko makubwa ya kuhakikisha Irain haiwezi kumiliki silaha za nyuklia ambapo zimefanikiwa kuingia nayo makubaliano mara kadhaa.

Tunafahamu kuwa uwezo wa kumiliki silaha za nyuklia ambao wanao Iran ulitokana na Urusi. Tunafahamu kuwa Urusi ilianza utengenezaji wa silaha hizo huko Irak, kabla ya kuvurumushwa na kwenda Iran na baadaye Syria ambako kulikuwa na mpango wa kuweka silaha hizo.

Hata hivyo, wakati huu hali imekuwa tofauti, mapambano dhidi ya silaha za nyuklia yamekuwa makubwa, lakini Rais Mteule wa Marekani, Donald Trump, amekuja kubadilisha upepo wa sakata hilo, tangu wakati wa kampeni Trump alitangaza kutupilia mbali makubaliano ya kudhibiti silaha za nyuklia kati ya nchi yake na Iran pamoja na Jumuiya ya Ulaya.

Kitendo hicho kilikuwa na maana ya kuipa mwanya Iran kuendelea na mchakato wa kumiliki silaha za nyuklia ambazo zinatajwa kuwa hatari kwa usalama wa dunia.

Hata hivyo, swali la kujiuliza; ni kwanini dunia iwe kwenye hatari ya silaha za nyuklia iwapo Iran itamiliki licha ya nchi nyingine kuwa nazo? Bado halijapatiwa majibu swali hili zaidi ya kuzungusha maneno ambayo yameshindwa kutatua mzozo uliopo. Yapo madai kuwa kuruhusu nchi kumiliki silaha za nyuklia kunatishia amani ya dunia, ikiwa na maana inafaa nchi chache kuzimiliki silaha hizo. Aidha, tishio jingine linalotajwa ni silaha za nyuklia kuangukia mikononi mwa makundi ya kigaidi, jambo ambalo linahatarisha usalama wa dunia.

Mapema wiki hii, Trump alitangaza kuwa Marekani inapaswa kuimarisha zaidi uwezo wake wa silaha za nyuklia maadamu ulimwengu haujapata mwelekeo wa kimantiki kuhusu silaha za atomiki.

Trump hakutoa maelezo zaidi katika uwanja huo lakini msemaji wake, Jason Miller, amesema rais huyo mteule alikuwa akiashiria vitisho vinavyohusiana na uzalishaji na uenezaji wa silaha za nyuklia na udharura wa kukabiliana na vitisho hivyo hususani vile vya makundi ya kigaidi katika maeneo yenye machafuko.

Trump pia ametilia mkazo suala la kuongeza uwezo wa silaha za nyuklia wa kuzuia vitisho kabla ya kutendeka kama mojawapo ya njia muhimu za kuimarisha amani. Matamshi hayo ni ya kwanza rasmi kutolewa na rais mteule wa Marekani kuhusu silaha za nyuklia za nchi hiyo.

Kutangazwa mtazamo huo wa Trump sambamba na matamshi yaliyotolewa na Rais Vladimir Putin wa Urusi kuhusu uwezo wa silaha za nyuklia wa nchi hiyo ni jambo linalopaswa kupewa uzito mkubwa.

Wakati Trump akitamka hayo, mwenzake Rais Vladimir Putin wa Urusi, alitilia mkazo udharura wa kuimarishwa uwezo wa silaha za nyuklia na silaha za kimkakati za nchi yake na kubainisha kuwa Serikali yake inapaswa kuimarisha zaidi makombora yenye uwezo wa kufumua na kupasua mfumo wa kujikinga na makombora.

Wachambuzi wa masuala ya kisiasa za kimataifa wanaona kuongezeka nguvu za matamshi baina ya Marekani na Urusi juu ya kupanua na kuboresha uwezo wa kumiliki silaha za nyuklia ama ujuzi wa kukabiliana na makombora yoyote ni ishara ya kuingia nyakati mpya za umiliki wa silaha kali ambazo zitaangukia nchi washirika wao, hali ambayo itatoa mianya kwa makundi yasiyolengwa kuzinasa na kusababisha madhara kwa maisha ya mwanadamu ulimwenguni.

Kwa mujibu wa taasisi za ulinzi za Marekani na Urusi, nchi hizo mbili pekee ndizo nguvu mbili za nyuklia zinazomiliki silaha za kimkakati za nyuklia katika nyanja tatu za anga, nchi kavu na baharini.

Wataalamu wanasema inatazamiwa kuwa hadi kufikia mwanzoni mwa mwaka 2040, Marekani itakuwa imepanua na kuboresha silaha zake za anga, nchi kavu na baharini za nyuklia kwa kutumia gharama ya dola trilioni moja.

Silaha za nyuklia za kipindi cha vita baridi zingali sehemu muhimu sana ya kimkakati ya ulinzi ya Marekani na maofisa wa nchi hiyo wanasisitiza udharura wa kulindwa uwezo wa nyuklia wa nchi hiyo.

Inaonekana kuwa Marekani ambayo imekuwa ikidai kwamba, inafanya jitihada za kupunguza silaha za nyuklia kote duniani, sasa inaiweka dunia katika ncha ya vita ya nyuklia baada ya maofisa wa ngazi za juu wa jeshi la nchi hiyo katika kipindi cha utawala wa Barack Obama kusisitiza tena sera ya kufanya mashambulizi ya mapema ya silaha hizo.

Lakini Marekani chini ya Donald Trump, inaonekana kuwa na kusudio kubwa la kuimarisha na kupanua zaidi uwezo wa nyuklia badala ya kupunguza.

Jambo hilo linamaanisha kuwa Marekani na Urusi zinaingia kwenye ngwe nyingine ya mapambano kupitia silaha za nyuklia, huku ikifahamika kuwa nchi hizo zina vituo vingi vya kijeshi kwenye nchi washirika wao. Hali ambayo inaonyesha taswira tofauti na awali hivyo kuwa tishio tuendako.

China nayo ni mshirika wa Urusi ambaye anamiliki silaha za nyuklia, inatajwa kuwa vigumu kuizuia nchi hiyo kutoa ujuzi kwa washirika wake wengine kwenye nchi ya ulimwengu wa tatu au mataifa mengine ya bara la Asia.

Kauli ya Trump imekuja kwa kisingizio cha kuimarisha ulinzi wa Marekani, huku wachambuzi wakibainisha kuwa upo msuguano wa muda mrefu kati yake na Urusi ambayo ndiyo mlengwa wa suala hilo kuliko China.

Kwa upande wake Urusi na China zimetenga bajeti kubwa kwa ajili ya kuboresha silaha zao za nyuklia. Urusi itaboresha asilimia 70 ya silaha zake za atomiki hadi kufikia mwaka 2020 pamoja na maghala mbalimbali ya silaha. Hapo ndipo kauli ya Trump inapoibua uchochezi wa hali ya juu wa kusambaa teknolojia ya utengenezwaji wa silaha za nyuklia.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles