27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Trump amkingia kifua mwana mfalme Saudia

WASHNGTON, MAREKAN



RAIS Donald Trump amesema amejulishwa kuhusu mkanda wa sauti wa mauaji ya mwanahabari Jamal Khashoggi, lakini binafsi hatousikiliza.

“Ni mkanda wa maumivu, ni mkanda mbaya,” alikiambia Kituo cha Televisheni cha Fox News juzi.

Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) lilitoa hitimisho kuwa mwana mfalme wa Saudi Arabia, Mohammed bin Salman aliamrisha kutekelezwa kwa mauaji hayo, lakini Ikulu ya Marekani,  haijathibitisha uchunguzi huo.

Saudi Arabia imeziita taarifa hizo za CIA kuwa za uongo na kudai bin Salman hakuwa akifahamu lolote kuhusu mauaji hayo.

Khashoggi aliyekuwa kinara wa kuukosoa utawala wa kifalme wa Saudia, aliuawa ndani ya ubalozi mdogo wa nchi hiyo jijini Istanbul, Uturuki Oktoba 2, mwaka huu alipokwenda kuchukua nyaraka ambazo zingemwezesha kufunga ndoa na mchumba wake raia wa Uturuki.

Saudia inasema Khashoggi aliuawa katika operesheni haramu iliyotekelezwa na maofisa wake wa usalama.

Kutokana na tukio hilo, wanaomuunga mkono Trump ndani ya Bunge la Wawakilishi wanamtaka achukue hatua kali juu ya mauaji hayo.

Lakini kutokana na unyeti wa Saudia kama mshirika thabiti wa Marekani katika Mashariki ya Kati, Trump amekuwa mgumu katika kufanya maamuzi.

Trump amesema hana haja ya kusikiliza sababu ameshaelezwa juu ya maudhui ya mkanda huo.

“Ninafahamu kila kitu kilichomo ndani ya mkanda huo bila hata ya kuusikiliza,” aliiambia Fox.

Mkanda huo ambao unatajwa kuwa ni ushahidi mkubwa wa tukio hilo, umesambazwa na Uturuki kwa Marekani na washirika wake.

Katika mahojiano hayo, Tump alisema Mohammed bin Salman amemwambia kuwa alikuwa hajui lolote juu ya mpango na kutekelezwa kwa mauaji hayo.

Trump amedai kuwa yawezekana isijulikane kabisa nani alikuwa nyuma ya mauaji hayo.

Hata hivyo alisema tayari kuna vikwazo vimeshawekwa juu ya wale wanaoshukiwa kutekelza uovu huo.

“Lakini wakati huo huo tunaye mshirika na mimi nataka nishikamane na mshirika ambaye kwa namna nyingi tu amekuwa mwema,” alisema Trump.

Hata hivyo, mahojiano ya Trump na Fox yalifanyika kabla ya kuvuja kwa ripoti ya CIA.

Japo CIA hawakutoa ushahidi wa moja kwa moja juu ya uhusika wa bin Salman kwa mauaji hayo, maofisa wa shirika hilo wanaamini tukio kama hilo lisingeweza kufanyika bila ruhusa yake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles