24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Trump aahidi kuangamiza uhalifu Marekani

Donald Trump
Donald Trump

CLEVELAND, Marekani

MGOMBEA urais wa Chama cha Republican, Donald Trump, ameahidi kumaliza uhalifu na ghasia nchini Marekani iwapo atachaguliwa kuwa rais kwenye Uchaguzi Mkuu wa taifa hilo unaotarajiwa kufanyika Novemba mwaka huu.

Trump, alitoa kauli hiyo wakati akifunga Mkutano Mkuu wa siku nne wa chama chake wa kumsimika rasmi kupeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi wa urais.

BBC imemkariri Trump akisema kwamba hakuwezi kuwa na ufanisi bila kuwepo utawala wa sheria.

Katika muktadha huo, aliahidi kuchukua hatua kali kukabiliana na wahamiaji haramu ambapo alifafanua kwa kusema kwamba,  kwa sasa wahamiaji wanaruhusiwa kuingia na kuishi katika jamii za Marekani bila kuzingatia usalama wa umma.

Alijitanabaisha kuwa ni mkombozi na sauti ya wanyonge na watu waliosahaulika nchini Marekani na akajionyesha kama mtu mwenye sifa tofauti na mpinzani wake wa Chama cha Democratic, Hillary Clinton ambaye amemtafsiri kama fisadi na asiyewajibika.

Trump ambaye ni moja ya wafanyabiashara wenye ukwasi mkubwa duniani, ameelezea mrengo wake kuwa atakomesha sera ya kujenga mataifa na kufanikisha mageuzi ya Serikali kimataifa.

Alisema sera hiyo ndiyo chanzo cha matatizo yanayoshuhudiwa nchini Iraq, Libya, Misri na Syria, hivyo aliahidi kufanya kazi na washirika wote wa Marekani wanaotaka kuangamiza kundi la Islamic State.

Katika hitimisho la hotuba yake, aliituhumu China kwa wizi wa haki miliki za Wamarekani na kuieleza Beijing kama taifa lililohadaa zaidi katika thamani ya sarafu yake katika historia. Trump ameweka wazi dhamira yake ya kushauriana upya na washirika kuhusu mikataba ya kibiashara yenye faida kwa Marekani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles