Na HADIJA OMARY- LINDI
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Lindi, imekifunga kiwanda cha saruji cha Kilwa kinachomilikiwa na Kampuni ya Lee Bulding Material Ltd, baada ya kushindwa kulipa kodi.
Meneja wa TRA Mkoa wa Lindi, John Jofrey, amesema hatua hiyo imekuja baada ya maofisa wa mamlaka hiyo kufanya ukaguzi wa kushtukiza katika eneo hilo la kiwanda na kubaini uwepo kwa deni la shilingi milioni 89.
“Wafanyabiashara hao wamekaidi agizo la Serikali la kutakiwa kulipa kodi ya mali, ukaguzi zuio, VAT na uendelezaji ufundi stadi jumla ya shilingi milioni 89 kati ya milioni 193 walizokuwa wanadaiwa tangu mwaka 2014,” alisema Jofrey.
“Tumewapa maagizo, tumewahamasisha lakini bado wamekaidi agizo letu, uamuzi tuliochukua ni kufunga kiwanda kipitia wakala baada ya siku saba taratibu za kuuzwa mali zilizoko kiwandani,” alisema Jofrey.
Aidha, Jofrey amesema lengo la kufikia hatua hiyo ni kuhimiza wafanyabiashara kulipa kodi stahiki kwa wakati badala ya kusukumana na ametoa wito kwa wafanyabiashara hao kuacha kushindana na Serikali badala yake kuhakikisha wanalipa kodi kwa wakati.
Ismail Ally ni mwakilishi wa Kampuni ya Lee Building Material Kilwa, amekiri kulitambua deni hilo.
Kwa upande wa dalali wa TRA Mchinga Action Malt, Doment Likome, alisema wamepata idhini ya kuzuia mali za kiwanda hicho mpaka watakapolipa deni hilo.