27 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

TPB inavyojitoa kuboresha elimu nchini

Madarasa ya Shule ya Msingi Misray yaliyokuwa awali

Na MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

KWA muda mrefu Watanzania wamekuwa wakiunga mkono masuala mbalimbali yenye manufaa kwa umma ikiwamo kupitia taasisi mbalimbali. Kutokana na hali hiyo, zipo baadhi ya taasisi hizo zimekuwa mstari wa mbele katika kuchangia huduma za kijamii kwa lengo la kurejesha sehemu ya faida yake kwa wananchi.

Katika Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya mwaka 2017, Serikali imekuwa ikifanya maboresho katika sekta ya fedha kuanzia miaka ya 1990, ambapo utekelezaji wake umepitia awamu mbili ya Mpango wa Maboresho katika sekta ya fedha.

Maboresho hayo yalilenga kuifanya sekta ya fedha kuwa huria kwa nia ya kuimarisha mfumo wa soko la fedha. Matokeo ya maboresho hayo yalileta mabadiliko katika sekta ya fedha, ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa watoa huduma ndogo za fedha.

Kutokana na hali hiyo, Benki ya TPB Plc ni miongoni mwa benki kongwe hapa nchini, inayoendelea kufanya vizuri katika kukuza thamani na kufikia malengo yake ya kimkakati mwaka hadi mwaka.

Benki ya TPB Plc imeendelea kujipambanua kama benki inayotoa huduma za kibenki kwa Watanzania wenye kipato cha kati na cha chini, na imekuwa ikipanga na kutekeleza mikakati thabiti ili kuhakikisha wateja wake wote wanapata huduma bora, za kisasa na kwa gharama ambazo kila Mtazania anaweza kuzimudu.

Kutokana na hali hiyo, benki hiyo imeweka mikakati kadhaa ikiwamo kuunga mkono juhudi za Serikali kuelekea uchumi wa kati na wa viwanda kwa kuwaandaa wataalmu wa kesho ambao wataendesha uchumi wa nchi kupitia sekta ya elimu.

Mbali na kutoa huduma bora za kifedha lakini bado TPB imekuwa mstari wa mbele katika kurudisha fadhila kwa wateja wao.

Kila mwaka, TPB imekuwa ikitenga fedha kutokana na faida yake ili kuweza kuisaidia jamii, kwa kushiriki katika utatuzi wa changamoto zinazoikabili jamii, ikijikita katika maeneo matatu muhimu ambayo ni elimu, afya na ustawi wa jamii.

Kwa upande wa elimu, benki ya TPB imejikita katika kuboresha miundombinu ya shule kwa kujenga vyoo, ujenzi na ukarabati wa madarasa, uchangiaji wa madawati, samani pamoja na vitabu na madaftari.

Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, zaidi ya shule 20 zimepata msaada kutoka benki ya TPB upande wa elimu.

Hospitali na vituo vya afya mbalimbali nchini pia vimefaidika na misaada. Misaada iliyotolewa ni pamoja na ununuzi wa vitanda vya wagonjwa, mashuka, magodoro, vyandarua na vifaa tiba.

Katika mahojiano maalumu na gazeti hili, Ofisa Mtendaji Mkuu wa TPB, Sabasaba Moshingi, anasema bado wanaendelea kufanya jitihada ili kuhakikisha fungu linalotengwa kwa ajili ya kusaidia jamii linaongezwa kila mwaka ili kuweza kukidhi maombi ambayo benki yake inayapata kila mwaka.

“TPB tunaamini kwamba sera yetu ya kusaidia jamii inaenda sambamba kabisa na sera ya Serikali inayoongozwa na Rais Dk. John Magufuli.

“Tunaamini elimu na afya bora ndio misingi muhimu katika kujenga jamii yenye uwezo wa kujenga ustawi endelevu,” anasema Moshingi.

Madarasa ya Shule ya Msingi Misray baada ya kujengwa na Benki ya TPB

Akizungumzia miradi wanayojihusisha nayo, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa TPB,  Noves Moses, anasema kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, benki imehakikisha inatenga fungu kwa ajili ya kutekeleza mradi mmoja mkubwa wa ujenzi.

“Mwaka jana, benki ilijenga madarasa mawili, ofisi ya walimu, vyoo vya wanafunzi pamoja na kuchangia madawati 50 kwenye shule ya Msingi Kitembere huko Serengeti, wilayani Bunda, Mkoa wa Mara.

“Vilevile mwaka huu, benki imejenga madarasa mawili, ofisi ya walimu pamoja na kuchangia madawati 50 kwenye shule ya Msingi Misray, iliyopo Kata ya Hondomairo, wilayani Kondoa.

“Hii ni moja ya miradi ambayo benki ya TPB inajivunia, kwani tumeweza kuwatoa watoto ambao hapo awali walikuwa wakisomea kwenye madarasa duni yaliyojengwa kwa udongo na kuezekwa kwa nyasi na kuwapatia jengo zuri la kisasa pamoja na madawati, hii ni fahari kubwa sana kwetu,” anasema Noves.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles