KOCHA wa zamani wa timu ya Toto Africans ya Mwanza, John Tegete, ameshangazwa na kitendo cha uongozi wa timu hiyo kuvunja naye mkataba kienyeji wakati akiwa amebakiza mwaka mmoja katika kandarasi yake.
Tegete ambaye aliinusuru klabu hiyo kushuka daraja msimu uliopita kwa kumaliza ligi kwenye nafasi ya 13 ikiwa na pointi 30, mkataba wake na Toto Africans ulitarajiwa kumalizika mwakani.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Tegete alisema kwamba anafikiria kuchukua hatua baada ya uongozi wa klabu hiyo kukaa kimya juu ya hatima yake ya kuendelea kukinoa kikosi hicho.
“Naweza kusema kwa sasa sina timu, Toto wanadai hawanitaki bila kutoa sababu za msingi lakini mkataba wangu unaisha 2017.
“Hata hivyo, kama hali itakuwa hivyo sifikirii kuifundisha timu yoyote hadi msimu ujao umalizike kwani nataka kupumzika,” alisema Tegete.