23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

TANZANITE YAHITAJI MKAKATI MAHUSUSI SOKONI

Na Shermarx Ngahemera


TANZANITE ni mwiba kwa masuala ya madini Tanzania na ina umaarufu wa kipekee kwa sababu madini hayo ya vito yanapatikana nchini pekee na hivyo kubeba mnyambuliko wa jina la nchi.

Ni fahari na heshima kwa nchi lakini ni aghalabu kukuta Watanzania wa kawaida wanayajua madini hayo yalivyo na hivyo kukosa ulinzi wa kwanza kutoka kwa wananchi wenyewe. Ni aibu kubwa na Serikali inabidi  ifanye juhudi kurekebisha kasoro hiyo ya wazi.

Kama nchi Tanzania inahitaji kufanya marekebisho mengi ili eneo hilo  la Kata ya Naisinyai linalotajwa kuwa na Tanzanite nyingi lakini cha ajabu nchi  nyingine  hasa Kenya, Afrika Kusini na India ndizo zinaendelea kunufaika huku Serikali ikipata asilimia tano tu inayotokana na madini hayo kama mrahaba wakati rasilimali ni yake. Kwanini ile rojo badala ya dikodiko?

Tokea ugunduzi wa madini hayo miaka ya sabini na Juma Ngoma wa Makanya watu wengi wamewahi kukamatwa na wengine kufungwa au kupoteza maisha katika awamu zote tano za utawala wa nchi yetu na hivyo kuendelea kuwa maarufu kwa mema na mabaya.

Kuna watu wengi wana kesi mahakamani  na mauaji mengi yametokea chanzo kikiwa tanzanite. Tukubaliane na hali hiyo kwani Waingereza wanaamini kuwa palipo na hazina hapakosi uhalifu, vitu hivi hutangamana kwani Mirerani na vitongoji vyake vimeshamiri uhalifu na dhuluma ya kila namna.

Msimamo huo anao hata Rais Magufuli na aliuelezea kwa kina alipokuwepo kata ya Naisinyai wilayani Simanjiro eneo la  mji mdogo  wa Mirerani katika ufunguzi wa barabara ya lami  ya urefu wa kilomita  26 kuelekea eneo hilo la utajiri mkubwa wa madini ya tanzanite na vito vingine vya sapphire, green tourmaline na graphite kwani kabla ya tanzanite (zoisite kwa jina lake la kikemikali) eneo hilo lilikuwa muhimu kwa  uchimbaji wa ‘graphite’ kama koti la kufichia mali.

Akiwepo Naisinyai  Rais  Magufuli  pia aliviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuwaachia wawekezaji ‘wenye umuhimu’ katika migodi ya Tanzanite ili wakakae na kamati ya kujadili madini chini ya Waziri wa Sheria na Katiba kurekebisha mkataba uliopo uwe na faida kwa Serikali na si wa kiunyonyaji pekee.

Wawekezaji hao walikamatwa hivi karibuni kwa ajili ya kusaidia kutoa taarifa nyeti kuhusu madini ya Tanzanite na Kampuni ya Tanzanite One ambayo baadaye ilionekana hata usajili wa kampuni yao ulitiliwa shaka.

Rais Magufuli hakumung’unya maneno pale aliposema kinagaubaga  kuwa wizi umetamalaki kwenye biashara  na uchimbaji wa Tanzanite.

“Sina sababu ya kumung’unya maneno, madini ya Tanzanite yanaibwa sana, ni shamba la bibi; tena la mabibi waliokufa miaka mingi kama vile hakuna mwenyewe,” alisisitiza.

“Watu wanachukua kuliko hata shamba la bibi. Mgodini kuna wawekezaji wameingia ubia na Shirika la Madini la Taifa (Stamico) kila mtu ana asilimia 50, lakini bado mali inasombwa na Serikali kugeuzwa  kuwa mtazamaji,” alisema Magufuli kwa masikitiko na kushangaa njama  na hujuma hizo.

Kutokana na hujuma inayofanyika  kwenye Tanzanite, Wakurugenzi wa Kampuni ya Tanzanite One, Faisal Juma na Hussein Gonga, wanaochimba Tanzanite kwa ubia na Stamico, walikamatwa kwa mahojiano ikiwa ni siku chache tangu Kamati ya Bunge itoe taarifa yake ya  uchunguzi wa madini hayo  na yale ya almasi iliyosomwa mbele ya Rais Dk. Magufuli, Ikulu Dar es Salaam ambayo  iliibua uozo na hujuma nyingi katika mwenendo mzima wa madini hayo mawili unaofanana na ule wa makinikia ya Acacia.

Karibu wadau wote walionekana kuihujumu Serikali kwa namna moja au nyingine. Alitoa  wito kwa vyombo husika ikiwamo Stamico. Benki Kuu, wawekezaji  na vyombo vya ulinzi na usalama  kuanzisha mustakabali mpya wa utendaji kazi kuinufaisha Serikali na jamii yote kwa ujumla.

Stamico iliyolazwa

Akielezea ushiriki wa shirika hilo kusimamia madini ya tanzanite kwa kufanya  biashara  badala yake kama  mwakilishi na hivyo mbia kwa  Tanzanite One, Rais Magufuli aliagiza  watu walioshiriki kufanya mambo ya  ovyo waondolewe mara moja kwani waliingia njama na upande mwingine kuidhulumu Serikali kwa kutokuwa makini na kuanza kujinufaisha  wao  binafsi.

Rais  alisema kama Taifa  inabidi kujipanga  upya na vizuri. Akaagiza vyombo vya ulinzi, polisi na usalama kuwa vihakikishe madini ya Tanzanite haivushwi  kinyemela na ovyo  ovyo ila kuwashughulikia  wote wanaoendesha hujuma hiyo. Hayo yalisikika na kushuhudiwa mubashara  kwenye redio na runinga zote nchini.

“Atakayetoka na Tanzanite kwenda nje ya nchi iwe halali amelipia kila  kitu  na aende zake salama  na apewe vibali sahihi.” Alipambanua mustakabali wanchi na kudai mabadiliko.

“Tupokwenye vita kubwa ya kubadilisha hii nchi, tumechezewa mno  na yale ninayoyaona kule  Ikulu ni maajabu mengi. Ikumbukwe kuwa nilipoingia madarakani mnafahamu tulifanya nini watumishi, wanafunzi, tumekuta hewa,” alieleza Rais kwa masikitiko makubwa.

Benki Kuu

Kwa mara nyingine, aliiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kutengeneza mkakati wa kushiriki ununuzi wa tanzanite kwa sababu  madini hayo si rahisi kudanganya kama inavyoweza kufanywa kwenye dhahabu. Alitaka benki iwe macho kulinda rasilimali za taifa na si fedha tu kwa kuwa wabunifu kutambua na kubaini mianya ya upotevu  wa mapato  kama  benki ya uwekezaji na sio ‘central bank pekee’. Ni benki inayotunza  hazina ya serikali kwa maana ya fedha, vito na rasilimali muhimu na adimu za umma kwa faida ya umma wenyewe.

Wawekezaji

Rais Dk. Magufuli, alisema  anawakaribisha  wawekezaji  kuja nchini  na Serikali inawahitaji wawekezaji wenye nia njema na si wawekezaji wanaopanga kuiibia nchi  na kujinufaisha wao pekee. Anataka faida kwa wote.

“Kama kutakuwa na mwekezaji anayetaka kuja nchini kutuibia basi huyo asije kabisa atakuwa amekula wa chuya kwani wakati huu hataiba bali atalia. Na hili nalisema kwa wazi, tumeamua kupambana kwa vita ya uchumi wa taifa letu.

“Nchi yetu ni tajiri, juzi tumekamata madini ya almasi yenye thamani ya fedha nyingi, kwenye madini ya dhahabu ndiyo usiombe ni uozo mtupu, ovyo,” alisema

Ujenzi wa ukuta

Katika  mazingira yasiyotegemewa na wengi  na kuonesha anakisimamia kile anachokisema na kuamini, Rais alifanya uamuzi  mgumu wa kujenga ukuta  kuzunguka eneo lote linalosadikiwa kuwa na madini hayo kam ule ukuta wa Kibiblia wa Jerusalem au ule Ukuta Mkuu wa China (The Great Wall).

Anataka biashara ya madini ya vito iwe rasmi kwa wahusika wote ili kujua nani anafanya nini na mapato hayo ili Serikali  ipate kodi yake bila kutumia nguvu nyingi na kwa uhakika zaidi kwa kurasimisha mengi yanayohusu madini hayo. Mifumo ikiwa madhubuti na rasmi itawezesha upatikanaji  mapato sadifu  na  ya kutosha .

Kama Kamanda  Mkuu wa Majeshi  ya Ulinzi na Usalama wa Tanzania akaliagiza  Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia  kuisimamia SUMA JKT kuanza haraka ujenzi wa ukuta katika eneo lote la uchimbaji wa Tanzanite kutoka vitalu A mpaka D, lenye eneo la kilomita za mraba 81.99. Baada ya siku tatu wanajeshi wakafika na kupiga kambi eneo husika na kuendelea na utekelezaji wa mradi huo wa ujenzi wa ukuta kama Kamanda Mkuu alivyoamrsisha.

Wadadisi wa mambo wanataka  tathmini sadifu ifanyike kwenye madini hayo isije ikawa yale ya ‘rhodolite’ kujirudia ambayo ilikuwa adimu na haipatikani lakini baadaye Brazil ikagundua machimbo  kwa uwingi ambayo yakafanya madini hayo kukosa thamani. Malkia Elizabeth aliyatumia madini hayo na kuweka mbele ya taji lake (crown) kitu ambacho  sasa anakiona kuwa dhalili  na kupunguza thamani halisi ya taji lake.

Kwa vile Tanzanite ina historia fupi isije ikatokea kama ilivyotokea kama kwa ‘rhodolite’ iliposhuka thamani yake na kufanya  uwekezaji  wa ukuta  kuonekana  kuwa hatukuwa  makini katika  kushughulikia kikamilifu suala hilo muhimu kiuchumi.

Rais Magufuli aliyeonekana kuumizwa na hujuma ya wizi wa Tanzanite, alisema ameona ni vema kuanza na hatua hiyo huku akiwa na matumaini kuwa mwekezaji wa Tanzanite One na wawekezaji wengine watakaa na Serikali kutengeneza mkataba mwingine wenye  faida kwa pande zote mbili zinazohusika.

Suala hili ni kuntu baada ya Profesa Palamagamba Kabudi ambaye ni Waziri wa Sheria na Katiba kukamilisha mazungumzo ya mapitio ya mikataba ya madini yenye mafanikio makubwa kwa  nchi kuhusu suala zima la madini na makinikia.

Rais anataka mkataba mpya kwa uchimbaji wa Tanzanite ili wadau wawajibike vilivyo.

“Wapitie kwa pamoja mkataba huu waurekebishe wasaini upya ili asilimia kubwa ya fedha zibakie hapa. Fedha hizo zitakapopatikana tuanze mpango wa kuweka maji na miundombinu mingine ya umma ya uhakika hapa Simanjiro.” Alisisitiza kutokea mabadiliko katika mahusiano  na mali hiyo kunufaisha zaidi wanyonge.

“Nimesema hapana, ndani ya mamlaka yangu lazima tujipange vizuri. Hili suala naona linafikia mwisho, tumechezewa vya kutosha. Najua kulikuwa na watu wanafaidika, biashara ya Tanzanite haijazuiliwa bali tunaitoa kwenye magendo na kuwa biashara halali.

Simanjiro vs Arusha

Arusha ni tanzanite na tanzanite ni Arusha, ni msemo ambao Rais anataka kufanyia mabadiliko na badala yake iwe Simanjiro ni tanzanite.

“Nataka Tanzanite iwe halali na si haramu, wachimbaji wadogo chimbeni, ukipata mali yako ukiwa ndani ya uzio kauze unavyotaka. “Tunataka soko la Tanzanite liwe Simanjiro si Arusha, wanaotoka Marekani na India waje wanunue hapa, akishuka na ndege hapo KIA aje kwa gari hapa anunue Tanzanite akauze anakojua,” alisema.

Dhana ya Arusha kama Blue City ikiwa na maana ya rangi ya tanzanite inabidi ipitiwe upya  kwani kwa muda mrefu watu wa Simanjiro wamenyonywa na wale wa Arusha wakati madini hayo ni mali hayo na kuamrisha minada ifanyike Mirerani na kuipa Mirerani hadhi ya Mji wa uwekezaji wa EPZA na kutaka Wizara husika kutekeleza  yanayotakiwa kufanifanikisha maamuzi hayo ili haki itendeke kwa watu wa Mirerani.

Alishangazwa na kitendo cha  kuona mji wa Mirerani uko nyuma kimaendeleo ya mengi  wakati  ndio eneo mama kwa madini  adimu ya tanzanite ambayo   duniani yanapatikana  katika Kata hiyo tu. Aliingiza matakwa ya Mungu kwa suala  hilo akiuliza na kutoa majibu mwenyewe.

“Hivi ni kwa nini Mungu atupe Tanzanite sisi peke yetu halafu hata gari la wagonjwa hamna? Hiyo gari nitawaletea mimi, na kuhusu suala la maji hilo pia niachieni nalifanyia kazi,” alisema Magufuli.

Viongozi waliokuwepo akiwamo Mbunge  Millya aliyepewa nafasi ya kuzungumza kwenye mkutano huo pamoja na wabunge wengine kutoka mikoa ya Manyara na Arusha, walimuomba Rais Magufuli kuhakikisha anaacha alama ya uongozi wake katika maisha ya wananchi wa Simanjiro.

“Nawashukuru kwa kumchagua Millya, ni mchapakazi amelelewa na CCM…ukimwona sura yake ni kama Chadema lakini moyo wake ni CCM kabisa,” alisema Magufuli huku akisisitiza kwamba ujenzi wa ukuta  Mirerani utakuwa na kamera  (CCTV) na vifaa maalumu vya kubaini wizi wa madini hayo.

Magufuli alisema kutakuwa na mlango mmoja wa kuingilia ili kudhibiti utoroshaji. “Hata ukimeza Tanzanite tumboni au kuficha kwenye viatu, itaonekana. Ndugu zangu viongozi waliopewa mamlaka ya kusimamia rasilimali hizi kama wangezisimamia vizuri leo hii Watanzania wasingekuwa masikini.”

Alishangaa kwa ufisadi kutawala maeneo mengi ya utendaji  kazi.

“Kubwa linafanyika kwa sisi viongozi tunaopewa mamlaka ya kusimamia tunakuwa sehemu ya mafisadi wa kuwaumiza Watanzania masikini, viongozi tunasahau tulikotoka, tulipo na tunakokwenda. Tanzanite hii haitakaa miaka yote, katika uongozi wangu nimeamua kuiongoza hii vita.”

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles