25.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Tanzania yawasilisha UN ripoti ya utekelezaji Maendeleo Endelevu

Saidina Msangi- New York

WAZIRI wa Fedha na Mipango Dk. Philip Mpango, amewasilisha ripoti ya Tanzania kwa mara ya kwanza ya mapitio ya hiyari ya utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu katika mikutano ya Jukwaa la Juu la Kisiasa la ngazi za mawaziri chini ya Umoja wa Mataifa (UN) New York nchini Marekani.

Akiwasilisha ripoti hiyo, Dk Mpango alisema Tanzania imefanikiwa katika utekelezaji wa malengo 17 yaliyoamuliwa kutekelezwa na nchi zote ulimwenguni ili kuondokana na umasikini na kuharakisha maendeleo.

Akizungumzia lengo namba nne lenye kuangazia elimu jumuishi na bora kwa wote, Dk. Mpango alisema Tanzania imepiga hatua katika uandikishaji wa wanafunzi wa darasa la kwanza.

Pia alisema Tanzania imefanikiwa katika maeneo ya utoaji huduma bora za afya, uongozi bora na amani ya nchi kwa ujumla.

 “Malengo haya ndio dira ya maendeleo na yanaunganika na mipango yetu ya maendeleo kwa pande zote za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yanaendana na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano, na Mkuza  kwa upande wa Zanzibar hivyo ni lazima tutekeleze malengo haya kwa bidii,” alisema Waziri Mpango.

Dk. Mpango alitoa wito kwa Jumuiya ya Umoja wa Mataifa na nchi zenye utaalamu kuisaidia Tanzania katika matumizi ya teknolojia ili kuweza kufikia azma ya malengo endelevu upande wa utunzaji wa mazingira.

Aliwashukuru  wadau wote, sekta binafsi na taasisi zisizo za kiserikali kwa ushiriki wao katika kuandaa ripoti hiyo kwa kiwango kizuri.

Aidha alitoa wito kwa taasisi na sekta binafsi kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha kuwa rasilimali fedha na utaalamu zitumike kwa ajili ya kushughulikia utekelezaji wa malengo endelevu.

Tanzania imeungana na nchi zote duniani katika utekelezaji wa malengo 17 yaliyoazimishwa  miaka minne iliyopita  ikiwa ni mkakati wa kufikia  ajenda ya 2030 ya maendeleo endelevu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles