30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

TANZANIA YACHAFULIWA BURUNDI

1NA ELIYA MBONEA, ARUSHA

*Yatuhumiwa kupitisha silaha bandarini Dar es Salaam

*Wanaharakati wamwangukia Magufuli, Mbunge Kimbisa adai ushahidi

RAIS Dk. John Magufuli ameombwa kuzuia upitishwaji wa silaha za kivita zinazodaiwa kupitishwa katika Bandari ya Dar es Salaam kwenda nchini Burundi.

Ombi hilo lilitolewa mjini hapa jana na vyama sita vya wanaharakati wa haki za binadamu na kiraia vilivyowasilisha
maombi yao mbele ya Kamati ya Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) inayoendelea kusikiliza maombi hayo mjini hapa.

Wanaharakati hao wameiambia Kamati hiyo ya Bunge kwamba, silaha hizo zinazodaiwa kupitia nchini Tanzania
hutumiwa na Serikali ya Burundi yakiwamo makundi ya vijana wanaodaiwa kuiunga mkono Serikali.

Mbele ya Kamati ya Migogoro na Usuluhishi ya Bunge la Afrika Mashariki, Rais wa Muungano wa raia wa Burundi wanaopinga muhula wa tatu wa Rais Pierre Nkurunziza, Vilalis Nshihirimana, alidai silaha hizo zimechangia umwagaji wa damu nchini humo.

Alisema zipo taarifa za uhakika kuwa silaha hizo zimekuwa zikipitia Dar es Salaam ambako kwa nchini Burundi hali
ya usalama imeendelea kuzorota huku mauaji ya raia wasio na hatia yanayofanywa na vyombo vya Serikali ikiwamo polisi, jeshi na makundi ya vijana yakiendelea kushamiri.

“Tunamuomba Rais Magufuli na Serikali ya Tanzania wazuie silaha hizo kuingia Burundi kupita Bandari ya Dar
es Salaam,” alisema Nshihirimana na kuongeza:

“Taarifa hizi za silaha kuingia Burundi kupitia Dar es Salaam ni za uhakika na tumezipata kutoka kwa watoa taarifa
wetu ambao tunalazimika kuwalinda lakini ni kweli silaha zinaweza kuingizwa kwa kupitia hata ndege zinazoenda
Burundi lakini ni wajibu wa kila mmoja wetu kuhakikisha kuna usalama wa kutosha kwa wananchi wa Burundi,” alisema.

Kwa upande wake Mbunge wa EALA, Dora Byamukama kutoka nchini Uganda, aliomba kupewa ushahidi wa tuhuma hizo.
Naye mbunge wa EALA kutoka nchini Burundi, Hafsa Mossy, aliwataka walalamikaji hao kueleza silaha hizo ziliingizwa na akina nani na kuwataka kuzungumzia silaha zilizozagaa na zinazotumiwa kushambulia miundombinu na maofisa wa Serikali zinatoka wapi.

Kwa upande wake Mbunge wa EALA kutoka Tanzania, Adam Kimbisa, aliwataka wanaharakati hao kuacha kutoa kauli zisizo na ushahidi na zinazoweza kuvuruga uhusiano baina ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

“Haya madai ni very sensitive (nyeti mno) na isitoshe hayana ushahidi wowote kwa kuwa hakuna arms embargo
(vikwazo vya silaha) ilivyowekewa Burundi na pia silaha zinaweza kuingizwa hata kwa kutumia usafiri wa ndege, sasa tusianze kunyoosheana vidole wakati tunatafuta suluhu ya mgogoro wa jirani zetu,” alisema Kimbisa.

Wanaharakati hao wanawasilisha maombi kwa Kamati hiyo ya Bunge la EALA ya kutaka Bunge hilo likutane kujadili
na kuutolea azimio mgogoro wa kisiasa unaoendelea nchini Burundi tangu Aprili mwaka jana baada ya Rais Nkurunziza kutangaza azma ya kuongeza muhula wa tatu wa kuiongoza nchi hiyo.

Wakati wanaharakati hao wakitoa madai hayo dhidi ya Tanzania, mwishoni mwa mwaka jana Serikali ya Burundi ilidai kukamata silaha nyingi kutoka kwa wafuasi wa upinzani.

Ilidaiwa kuwa waliokamatwa ni wafuasi wa chama kikuu cha upinzani cha FNL kinachoongozwa na Agathon Rwasa.
Kukamatwa kwa silaha hizo kulitokana na kundi la watu wenye silaha kudaiwa kuingia nchini humo.

Ilidaiwa wakati watu hao wakikabiliana na jeshi la nchi hiyo katika Mkoa wa Kayanza, Kaskazini mwa Burundi, polisi walifanikiwa kukamata bunduki thelathini katika kijiji kimoja cha Mkoa wa Muyinga, Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo.

Siku chache baadaye polisi hao hao walidai kukamata silaha nyingine kutoka kwa vijana wa chama tawala cha CNDD-FDD.
Kumekuwa na mapigano ya mara kwa mara nchini Burundi kati ya kundi la watu wenye silaha na vikosi vya usalama na jeshi la nchi hiyo.
Pamoja na kwamba vyombo vya usalama vimekuwa vikidai kudhibiti hali hiyo, hata hivyo uchaguzi uliomuingiza
madarakani Rais Nkurunziza hivi karibuni umeamsha hasira kubwa hususani kutoka kwa wapinzani wake na hivyo kuzua hali ya shaka.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles