28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Tamwa yateta na wajumbe Bunge la Katiba

Valerie Msoka
Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Valerie Msoka

Na Oliver Oswald, Dar es Salaam

CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kikishirikiana na Mtandao wa Wanawake na Katiba, jana walikutana na wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba na kujenga kwa pamoja mikakati endelevu ya kutetea masuala ya haki za wanawake na usawa wa kijinsia katika Katiba Mpya.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana na Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Valerie Msoka, ilieleza mkutano huo utawapa fursa wana mtandao na wajumbe wa Bunge hilo kwa kuweka nguvu zaidi katika uelewa wa masuala ya haki za wanawake kikatiba.

Msoka alisema mbali na hili pia ni moja ya njia za kuhakikisha misingi ya usawa wa jinsia inazingatiwa katika kipindi cha pili cha majadiliano katika Bunge Maalumu la Katiba, kinachotarajiwa kuanza Agosti 5, mwaka huu.

“Mtandao unaamini kuwa wajumbe wa Bunge la Katiba wakiwa na nia ya pamoja, wanaweza kuleta Katiba itakayolinda, kutetea na kuheshimu misingi ya haki na usawa wa jinsia kwa taifa zima.

“Mkutano huu ni mwendelezo wa mikakati ya TAMWA na Mtandao wa Wanawake na Katiba katika kujenga uelewa na umuhimu wa masuala ya wanawake katika Katiba Mpya, kwani mikutano mingine imefanyika mjini Dodoma na Dar es Salaam tangu Bunge Maalumu lilipoanza vikao vyake,” alisema Msoka katika taarifa yake.

Mtandao wa wanawake ni muungano wa Taasisi mbalimbali za wanawake zinazopigania haki za wanawake nchini. Mtandao huu unaratibiwa na Taasisi ya WFT, TAMWA, TAWLA, SWAUTA, TGNP, EFG, HAWA, KWIECO, ULINGO,) TWCP, TUWODEA.

Taasisi nyingine ni WLAC, ZGC, KIVULINI, Wote Sawa, Jitolee Kishapu, ADC Foundation, SAWATA, ZAFELA pamoja na Jukwaa la Katiba na Wanawake Wanaharakati Binafsi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles