ADDIS ABABA, ETHIOPIA
MWENYEKITI wa Kamisheni inayosimamia mchakato ulioshindwa wa utafutaji wa amani nchini Sudan Kusini, Festus Mogae amesema nchi hiyo haipaswi kupoteza fursa ya upatikanaji amani katika mkutano ujao.
Licha ya makubaliano kadhaa ya kusimamisha mapigano, bado machafuko yameendelea nchini humo tangu vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipoibuka mwishoni mwa 2013, miaka miwili tu baada ya taifa hilo changa kabisa duniani kujipatia uhuru wake.
Majeshi yanatomtii Rais Salva Kiir, yanapambana na yale yanayomtii Makamu Rais wa zamani, Riek Machar.
Maelfu ya watu wameuawa tangu kuanza kwa mgogoro huo huku taifa hilo likikabiliwa na upungufu mkubwa wa chakula.
Hata hivyo, Serikali na makundi ya waasi walitia saini mpango wa kusitisha mapigano mjini Addis Ababa, Ethiopia, Desemba mwaka jana wakinuia kufufua makubaliano yaliyotiwa saini mwaka 2015.
Makubaliano hayo yalikiukwa saa kadhaa tu baada ya kutiwa saini.
Kwa sasa pande husika zitakutana tena mjini hapa Mei 17 hadi 21 kujaribu kuanzisha tena mchakato wa kutafuta amani ulioandaliwa na Jumuiya ya Ushirikiano wa Maendeleo ya Nchi za Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika (IGAD).
“Nchi hii imekosa nafasi nyingi za kuhakikisha kunakuwepo na amani ya kudumu na hatupaswi kukubali mkutano mwengine upoteze fursa hii,” alisema Mogae, Rais wa zamani wa Botswana katika hotuba yake.
Nchi hiyo pia imeanza mchakato wa mazungumzo ya kitaifa wakati mapigano yakiendelea nchini humo.
Mogae amezishutumu pande hasimu kwa kukiuka haki za binadamu huku akiihimiza IGAD kuwachukulia hatua wale wote wanaoyumbisha au kuharibu makubaliano hayo.