23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Sorrry Klopp…! tukutane mwisho wa msimu

ADAM MKWEPU NA MITANDAO

LIVERPOOL  haina jeuri tena ya kuweka rekodi ya kunyakua ubingwa wa Ligi Kuu England  bila  kufungwa, badala yake imewapa nafasi Manchester City kuwa na matumaini ya kulitetea taji hilo hadi mwisho wa msimu.

Katika mchezo wa 21 wa Ligi Kuu England, Liverpool imeruhusu kufungwa mabao 2-1 na Manchester City, hivyo haitaweza kufikia rekodi ya Arsenal ya msimu wa 2003/04 ambao walikuwa mabingwa bila kufungwa.

Liverpool inaongoza ligi ikiwa na  pointi 54 wakati Manchester City ikipaa hadi nafasi ya pili na pointi 50, baada ya timu zote kucheza michezo 21 na kufanya  ubingwa wa ligi hiyo kuwa wazi kwa timu tatu za juu ikiwamo Tottenham yenye pointi 48 ikiwa na  idadi sawa ya michezo iliyochezwa na vinara hao.

Historia imeweka wazi kuwa timu inayoweza kufikisha pointi 50 hatua kama hii inaweza kunyakua taji hilo.

Kitendo hicho kilionekana kwa Chelsea ilivyonyakua taji hilo msimu wa 2005/06, Manchester United msimu wa 2006/07 na Manchester City 2017/18.

Kama Liverpool  ingeshinda  dhidi ya Manchester City wiki iliyopita katika Uwanja wa Etihad,  kusingekuwa na nafasi  kwa  timu nyingine kuwaza ubingwa huo  msimu huu kwa kuwa ingekuwa na  tofauti ya pointi 10 dhidi ya miamba ya Manchester.

Lakini kwa  sasa ubingwa wa ligi hiyo itategemea na matokeo ya  michezo 17 iliyobaki, ndivyo historia inavyoeleza namna gani itakavyokuwa ikiwa matokeo yatakwenda kama yalivyotokea wiki iliyopita.

Ni miaka 28 tangu Liverpool itwae ubingwa wa ligi hiyo na wengi watakumbuka namna ilivyokosa kunyakua taji hilo  msimu wa 2013/14 wakati timu hiyo ikiwa chini ya kocha Brendan Rodegers.

Baada ya kucharazwa na Chelsea taratibu iliondoka katika mbio za ubingwa na kuiachia Manchester City.

Ni muhimu kukumbuka tukio hilo licha ya kwamba Liverpool kwa sasa ipo katika ubora wa hali ya juu.

Tukio kama hilo lilitokea  msimu wa 1996/97 wakati Liverpool ikiwa chini ya Roy Evans na ikamaliza nafasi ya nne ikipitwa pointi saba na bingwa Manchester United iliyokuwa ikifundishwa na Sir Alex Ferguson.

Wakati huo kama kikosi cha Evans kingepata pointi nne katika michezo miwili kingeongoza msimamo wa ligi hiyo.

Kwa sasa Liverpool inatakiwa kuwajibika kuhakikisha pengo la idadi ya pointi iliyopo haipungui na kuwapa nafasi wapinzani wake.

Timu hiyo kwa sasa ipo kwenye presha ya kuhakikisha inafanya vizuri katika kila mchezo na pengine jambo hilo linaweza kuwagharimu kutokana na upinzani uliopo kwenye ligi hiyo.

Moja ya sababu ya Liverpool kucheza michezo 20 bila kufungwa ilitokana na ubora wao, hiyo inawafanya kuwa bora Ulaya na pengine duniani kwa sasa.

Ili kufanikiwa ilichokifanya katika michezo 20 iliyopita, Liverpool inatakiwa kutokata tamaa kuamini kwamba waliteleza na wanatakiwa kuinuka tena katika ubora wao.

Majogoo hao bado hatima ya ubingwa wa England upo kwenye  mikono yao, lakini wakiteleza tu itakuwa imekula kwao.

Taji kubwa ambalo Liverpool imelinyakua kwa sasa ni Kombe la FA msimu wa 2005/06.

Baada ya kumaliza msimu uliopita ikiwa nafasi ya nne ikitoka kupoteza mchezo wa fainali wa Ligi ya Mbaingwa Ulaya dhidi ya Real Madrid, imejaribu kuongeza nguvu kikosi chao kwa kusajili wachezaji kadhaa lakini wengi wao wanahitaji uzoefu.

Kikwazo kingine kinachonekana kwa Liverpool msimu huu ni wakati itakapokutana na Brighton, Crystal Palace , Leicester, West Ham, Bournemouth.

Februari 24 mwaka huu timu hiyo itavaana na Manchester United, ikiwa ni siku chache baada ya kucheza mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya  Bayern Munich.

Mzunguko wa pili Liverpool ilishinda dhidi ya Manchester United katika hali ya kutokuwa na presha lakini  kwa sasa mambo yamebadilika tangu  Jose Mourinho afukuzwe na nafasi yake kuchukuliwa na Ole Gunnar Solskjær.

Lakini  zaidi ni kwamba Manchester United wanatakiwa kuwa katika kiwango cha juu wakati wakivaana na PSG wiki moja kabla ya kuvaana na Liverpool.

Wakati huo Manchester City na Tottenham bado ratiba zao hazitakuwa na  presha, kwani vijana wa Pep Guardiola watakuwa wakivaana na Everton huku Tottnham ikivaana na  Burnley katika Uwanja wa Turf Moor.

Wiki moja baada ya kucheza dhidi ya Manchester United na siku chache baada ya kucheza dhidi ya Watford, ikiwa katikati ya wiki Liverpool itavaana na Everton katika Uwanja wa Goodison Park.

Liverpool inayo rekodi nzuri katika uwanja wa nyumbani uliopo mji mdogo wa  Merseyside wakati inapocheza dhidi ya wapinzani wake, lakini inapotokea  kucheza katika eneo tofauti matokeo yanakuwa tofauti pia.

Kwa Manchester City na Tottenham, zitakuwa zikivinjari huku wakitaka Liverpool ipoteze mchezo huo.

Lakini Manchester City italazimika kuifunga Bournemouth katika mchezo utakaochezwa Uwanja wa Vitality, wakati Tottenham ikiwa nyumbani ikitafuta pointi dhidi ya Arsenal.

Liverpool itavaana na Tottenham katika Uwanja wa Anfield Machi 30 mwaka huu,  hii ikiwa nafasi kwa Manchester City kuongoza ligi kwa mara nyingine.

Msimu uliopita vijana wa Klopp walifungana mabao 2-2 dhidi ya  Tottenham na hiyo inaonekana huenda ikatokea tena msimu huu katika hatua hii ya mzunguko wa pili.Wakati mchezo huo ukiendelea, Manchester City itakuwa ugenini ikicheza dhidi ya Fulham.

Kwa sasa Fulham ipo chini ya kocha mpya, Claudio Ranieri, huenda akabadilisha matokeo ya awali ambapo timu hiyo ilifungwa mabao 3-0 katika Uwanja wa Etihad.

Liverpool itamaliza presha ya michezo mikubwa wakati itakapovaana na Chelsea Aprili 13 mwaka huu. Miamba hiyo katika michezo yao iliyopita ilifungana bao 1-1 wakati zilipovaana Uwanja wa Stamford Bridge na matokeo hayo yanaweza kuzifurahisha tena klabu za Manchester City na Tottenham.

Katika wiki hiyo hiyo, Manchester City itakuwa ugenini ikicheza dhidi ya Crystal Palace.

Mchezo uliopita vijana wa Guardiola waliwafunga Palace mabao 3-2 katika Uwanja wa Etihad Desemba 22 mwaka huu huku Tottenham ikicheza dhidi ya Hudderfield.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles