33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

SIMULIZI YA KUHUZUNISHA ALIYEJIFUNGUA AKIWA POLISI

Na Ashura Kazinja – KILOMBERO


MWANAMKE mmoja mkazi wa Kijiji cha Mgudeni, Tarafa ya Mang’ula, Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro, Amina Mbunda (26), amelazimika kujifungulia kituo cha polisi baada ya kukosa msaada.

Hatua ya kujifungulia polisi kwa mama huyo, imetokana na uamuzi wa polisi wa Kituo cha Mang’ula kumweka mahabusu baada ya kumuhusisha na tukio la mumewe anayedaiwa kununua kitanda cha wizi.
Tukio hilo lilitokea Juni Mosi mwaka huu.

Mama huyo alikamatwa baada ya askari polisi kufika nyumbani kwake kwa lengo la kumkamata mumuwe ambaye alikuwa safarini.

Kutokana na kukosekana kwa mumewe, askari hao waliokuwa wameongozana na mgambo wa kijiji, walimchukua kwa nguvu hali ya kuwa tayari alishaanza kusikia dalili za uchungu.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Amina, alisema askari hao walifika nyumbani kwake saa tatu usiku wakati mama mkwe wake alikuwa amekwenda kutafuta pikipiki ampeleke hospitali kujifungua.

“Walikuja polisi na Andrew Songea, ambaye ni Mwenyekiti wa Kitongoji cha Makambale na mlalamikaji. Wakati huo nilikuwa na uchungu, nikawaeleza hali yangu, lakini hawakukubali wakanilazimisha kwenda nao kituoni kwa niaba ya mume wangu.

Alisema akiwa mahabusu, licha ya kulalamika kuumwa uchungu, askari wa zamu alimpuuza hadi alipoona amezidiwa na kumtoa nje alikojifungulia kwenye nyasi bila msaada.

“Walipokuja askari niliwaambia mume wangu hayupo na mimi naumwa, najisikia uchungu, hivyo nataka kwenda hospitali kwani hali yangu si nzuri na hapa nina dalili zote za kujifungua.

“Licha ya kuwaeleza, lakini askari hao waligoma na wakasema najifanyisha, hivyo waongozane na mimi hadi polisi hadi pale mume wangu atakapokwenda kujisalimisha.

“Tulipofika polisi niliwekwa mahabusu, muda ulivyokuwa ukienda, hali yangu ilizidi kuwa mbaya na hata nilipokuwa napiga kelele za kuomba msaada, askari walihisi natafuta huruma.

“Nilipambana na ile hali, kwa bahati mbaya askari wote waliokuwapo pale kituoni walikuwa wanaume, ilipofika saa tisa usiku, hali ilikuwa mbaya zaidi nikawaambia najifungulia humu ndipo walipokuja kufungua mlango na nikatoka nje pembeni ya kituo kuna majani, nikajifungulia hapo.

“Mtoto alidondokea kwenye nyasi ambako kulikuwa na baridi kali, sikuwa na kanga zaidi ya gauni iliyokuwa nimevaa,” alisema.

Alisema hata baada ya kujifungua, alikosa msaada wa haraka ikiwamo mtoto kutotoka kwenye kondo.
“Aliitwa mtu wa kwanza ambaye alisema hawezi ile kazi na baada ya muda walimwita mtu mmoja ambaye anaishi jirani na kituo cha polisi, ambaye naye alisema hawezi.

“Ndipo alipoitwa mama mwingine ambaye alinisaidia na baada ya muda nikapelekwa Kituo cha Afya Mang’ula ambako nililazwa na kupatiwa matibabu mengine.

Inaendelea…………… Kwa habari zaidi jipatie nakala ya gazeti la MTANZANIA.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles