26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Simba SC yaiamkia tena Stand United

THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

BAADA ya kupiga kambi ya muda Singida, kikosi cha Simba kimepanga kuondoka mkoani humo leo kwenda Shinyanga kwa ajili ya mchezo wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Stand United.

Simba itakuwa mgeni wa Stand United katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaopigwa kesho kutwa Uwanja wa Kambarage mkoani humo.

Simba itakutana na Stand United ikitoka kupata ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Lipuli FC, katika mchezo wake wa mwisho wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa Uwanja wa Samora, Iringa.

Akizungumza na MTANZANIA jana, kocha wa viungo wa timu hiyo, Aden Zrane, alisema kwa ujumla hali za afya za wachezaji wao ziko timamu.

“Tulifika juzi usiku Singida na leo (jana) jioni tutaendelea na mazoezi ya kujiandaa na mchezo wetu dhidi ya Stand United kisha kesho tutaondoka, tunafahamu bado tuna kazi kubwa ya kuhakikisha tunapata matokeo mazuri,” alisema Zrane na kuongeza:

“Wachezaji wetu wapo fiti kucheza mchezo huo isipokuwa Erasto Nyoni  ambaye ameshaanza mazoezi mepesi lakini hawezi kucheza kwa sasa,” alisema.

Zrane alisema kusudio lao ni kuendeleza rekodi ya ushindi katika mechi zao zinazowakabili mbele, hivyo wamejiandaa kwa mapambano bila kujali wanacheza nyumbani au ugenini.

“Wachezaji wote wana morali ya juu ukizingatia tumetoka kushinda michezo mfululizo, lazima tuongeze juhudi ili kupata pointi tatu nyingine ugenini,” alisema.

Simba inashika nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu, ikiwa na pointi 48, baada ya kushuka dimbani mara 19, ikishinda 15, sare tatu na kupoteza mchezo mmoja.

Yanga ndiyo inakamata uongozi wa ligi hiyo, ikiwa na pointi 61, baada ya kucheza michezo 25, ikishinda 19, sare nne na kupoteza michezo miwili, nafasi ya pili iko Azam FC yenye pointi 50, ikishinda 14, sare nane na kupoteza mara tatu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles