25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Simba, Messi hakijaeleweka

MESSI GOALNA ABDUCADO EMMANUEL, DAR ES SALAAM

MGOGORO wa kimkataba wa winga wa timu ya Simba, Ramadhan Singano ‘Messi’ na timu yake hiyo umezidi kutikisa baada ya pande hizo mbili kuendelea kuvutana.

Messi analalamikia mkataba wake kughushiwa kwa kuongezwa mwaka mmoja zaidi unaomalizika mwakani, tofauti na ule wa awali aliosaini yeye unaofikia tamati Julai mwaka huu.

Uongozi wa Simba umekuwa ukikana madai hayo ukidai Messi alisaini mwenyewe mkataba huo wa mwaka mmoja, kabla ya ule wa awali kumalizika baada ya kuboreshewa maslahi yake.
Sakata hilo la Messi kulalamika kughushiwa mkataba wake linafanana na lile la kiungo wa zamani wa Simba, Athuman Idd ‘Chiji’, ambaye pia alilalamika saini yake kughushiwa kipindi ambacho anataka kuihama klabu hiyo msimu wa 2007/2008.

Akizungumza na kituo cha Redio EFM kupitia kipindi cha asubuhi cha ‘Sports Headquarter’, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe, alisema Messi anatakiwa kuthibitisha ukweli wa jambo hilo kwa kuwapelekea mkataba halisi na sio kopi.

“Anaongea ongea hovyo hovyo kila mahali, anaichafua Simba, hizi ni tuhuma za jinai, sisi tumemwambia kama anaona kuna walakini kwenye mkataba tuliokuwa nao sisi, alete na yeye kopi yake ya mkataba ‘original’ (halisi) ili tulinganishe na tujue wapi kuna tatizo.”

“Messi ni kama mtoto wetu kwani tumemlea, sasa umeshawahi ona wapi mtoto anagombana na mzazi wake, sisi tumemsomesha na kumfanyia kila kitu hadi yupo hapa, hivi karibuni tulikuwa na mpango wa kumpeleka Australia akacheze, lakini kutokana na mambo yake haya tutasitisha hilo na tutaiambia hiyo klabu kwa sasa hatuwezi kumwachia, labda mpaka amalize mkataba mwakani na aende bure,” alisema.

Kamanda huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), alimshauri Messi kuwa kama anataka kuondoka Simba basi afuate taratibu, kwani wachezaji wao wote wako sokoni.

Aliongeza kuwa hawamtambui meneja wa Messi (Hamis Said), kwani si wao tu ambao hawana barua rasmi ya utambulisho wake, amedai hata Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na lile la Afrika (CAF) nao hawamjui.

“Sisi tunamjua wakala anayeitwa Kadito (Denis), hata TFF wanamjua na tumekuwa tukishirikiana naye sana, amekuwa akiwachukua wachezaji wetu na kutuletea wachezaji pia, hata yeye akikosea TFF inao uwezo wa kumshughulikia, sio huyu ambaye hajulikani na hajui anachoongea,” alisema.

Alipotafutwa Messi naye alisema hawezi kuutambua mkataba huo, anachoangalia sasa ni kusaini mkataba mpya utakaoboresha ule uliomalizika.

“Nilishawapelekea mkataba niliokuwa nao huo wa miaka miwili ulioisha na nimekuwa nikiandikia barua mara kwa mara kueleza namna mkataba huo ulivyokuwa ukikiukwa kama vile kutopewa kodi ya nyumba, bonasi,” alisema.

Alisema Desemba mwaka jana aliwahi kumuuliza Makamu wa Rais, Geofrey Nyange ‘Kaburu’, kuhusu kutopewa fedha za kodi ya nyumba kama mkataba unavyoeleza, alidai kujibiwa “mchezaji mzawa huwezi kulipwa kodi ya nyumba.”

Messi aliongeza kuwa baada ya ligi kuisha aliitwa kumaliza sintofahamu hiyo na kudai Simba ilikiri kupitia Kaburu kuwa kuna walakini kwenye mkataba huo, lakini hadi sasa hawajampa majibu ya kueleweka namna ya kulimaliza.

Aliongeza kuwa: “Watu wanadanganywa kwamba mimi nina tamaa ya fedha, jambo ambalo si kweli mimi nataka hili suala limalizike kabla ya taratibu nyingine kumalizika.”

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles