31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

SIMBA KIBOKO

  • Yaipiga Coastal Union na kuitibulia rekodi ya kutopoteza Mkwakwani
  • Yanga yadondokea pua kwa Mtibwa Sugar, yatunguliwa Jamhuri

MWANDISHI WETU-TANGA

MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba, imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Coastal Union, Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, wakati Yanga ikicharazwa bao 1-0 na Mtibwa Sugar Uwanja wa Jamhuri, Morogoro, michezo yote ikichezwa jana.

Matokeo hayo yanaifanya Simba kufikisha pointi 60 na kusalia nafasi ya tatu, lakini ikiwa na akiba ya michezo tisa mkononi dhidi ya vinara wa ligi hiyo Yanga, wanaokamata usukani wakiwa na pointi 74.

Wekundu hao wameshuka dimbani mara 23, wakishinda michezo 19, sare tatu na kupoteza mchezo mmoja, wakati Yanga imecheza michezo 32, imeshinda 23, sare tano na kupoteza minne.

Coastal Union ndiyo ilitangulia kupachika bao la kuongoza kipindi cha kwanza kupitia kwa Raizin Hafidh dakika ya kwanza, aliyetumia makosa ya beki wa Simba, Erasto Nyoni na kipa wake, Aishi Manula, kushindwa kuwasiliana vema.

Kipindi cha kwanza kilimalizika Coastal ikiwa mbele kwa bao 1-0.

Kipindi cha pili, Simba ilirejea uwanjani na mkakati mpya wa kusawazisha kwa kuongeza kasi ya mashambulizi langoni mwa wenyeji.

Jitihada za Simba zilizaa matunda dakika ya 49, baada ya mshambuliaji, Meddie Kagere, kuisawazishia kwa mkwaju wa penalti, baada ya Emmanuel Okwi, kuangushwa na kipa, Sudi Abdalah.

Kagere aliifungia tena Simba bao la pili dakika ya 67, baada ya kumalizia pasi ya Clatous Chama.

Dakika 90 za mchezo huo zilimalizika huku Simba ikiondoka na ushindi wa mabao 2-1.

Yanga licha ya kichapo ilichopata jana bado inaendelea kusalia kileleni mwa msimamo wa ligi na pointi 74, baada ya kucheza michezo 31, ikishinda michezo 23, sare tano na kupoteza michezo minne.

Bao pekee la ushindi la Mtibwa Sugar lilifungwa na Riphati Hamisi, dakika ya 52, akiwa eneo la hatari baada ya kupokea pasi ya Haruna Chanongo.

Kipigo hicho kilitosha kufifisha matumaini ya Yanga kuendelea na mbio za ubingwa msimu huu licha ya timu hiyo kuendelea kuongoza msimamo wa ligi hiyo.

Katika mchezo wa jana timu hizo zilimaliza kipindi cha kwanza zikishindwa kufungana huku Yanga ikionekana kukosa nafasi za wazi.

Dakika ya 70, Kelvin Kongwe wa Mtibwa Sugar, alionyeshwa kadi ya njano baada ya kumchezea rafu Abdalah Shaibu na dakika ya 80, Kihimbwa pia alionyeshwa kadi ya njano.
Amisi Tambwe, aliifungia bao Yanga dakika ya 85 baada ya kuunganisha kwa pasi ya kichwa krosi ya Mrisho Ngasa, lakini mwamuzi alisema mfungaji alikua ameotea.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles