27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

SIKU NANE ZA OBAMA SERENGETI

RAIS Barack Obama

nA WAANDISHI WETU, DAR NA ARUSHA

RAIS mstaafu wa Marekani, Barrack Obama amehitimisha ziara ya siku nane nchini akitumia muda mwingi katika Hifadhi ya Serengeti kwa kueleza kuwa imemfumbua macho na kuahidi kushawishi watalii zaidi kutoka nchini mwake kuja Tanzania.

Obama aliyekuwa katika ziara binafsi na familia yake alieleza kuvutiwa sana na maeneo ya utalii ndani ya Hifadhi ya Serengeti, akisema ni urithi wa aina yake na umemfumbua macho, tangu Jumapili iliyopita.

Obama ambaye alipokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Augustine Mahiga kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) jana, alisema atawashawishi Wamarekani kuja kuwekeza kwenye utalii na maeneo mengine.

Gazeti la MTANZANIA ndilo pekee lililoripoti ujio wa Obama, ambaye amekuwa kwenye hifadhi hiyo kwa usiri mkubwa huku mwenyewe akisema kuja Tanzania ni sawa na kurudi nyumbani na akaahidi kurejea tena.

Alikuwa akizungumza baada ya kutua kwa ndege ndogo kutoka Serengeti, kisha akabadili ndege tayari kwenda Nairobi, Kenya atakakokuwa na ziara ya siku moja kisha kuelekea nchini Afrika Kusini.

Katika hatua nyinge, Waziri Mahiga alimkabidhi barua na salamu kutoka kwa Rais Dk. John Magufuli Jumapili iliyopita wakati jana alimkabidhi zawadi kutoka kwa rais. Obama alishukuru kwa zawadi na salamu hizo.

Pia alimkabidhi zawadi ya kitambaa maalumu chenye picha ya wanyapori aina ya nyumbu ambao huwa wanatengeneza tukio la kihistoria na kuhama kila mwaka wakitoka Maasai Mara ya Kenya na kuingia Serengeti, zawadi hiyo pia ilitoka kwa Rais Dk. John Magufuli

Kwa upande wake, Meneja Uhusiano wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA), Paschal Shelutete alisema kuja kwa viongozi na watu mashuhuri kutembelea hifadhi za taifa ya Serengeti ni matokeo ya jitihada za TANAPA kutunza mfumo wa Ikolojia ya asili na hivyo kuwa kivutio kwa watu wengi wa nje na ndani ya nchi.

“Ujio wa viongozi mashuhuri kama Obama na wengineo kunatokana na jitihada za TANAPA za kuhakikisha mfumo wa Ikolojia unakuwa endelevu. Ni tofauti kabisa na mataifa mengine ambako wameshaharibu,” alisema Shelutete

Naye Meneja wa KADCO, Mhandisi Christopher Mukoma alisema ujio wa Obama katika zaiara binafsi ni dhihirisho kwamba KIA sasa inaweza kupokea wageni wa kila namna na ndege za kila aina na kwamba baada ya ukarabati mkubwa uliofanywa katika miundombinu ya uwanja huo, watalii wengi zaidi wataingia nchini.

Mhandisi Mukoma alisema Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) ambalo linafufuliwa na Serikali kwa kupewa ndege mpya Saba litakuwa katika nafasi ya kukua zaidi kwa kutumia uwanja huo na kukuza utalii, kwani KIA ni lango la utalii kwa ukanda wa Kaskazini.

Hifadhi ya Taifa ya Serengeti aliyoitembelea Rais Obana  ipo kwenye maajabu saba ya duniani, ikiwa na vivutio mbalimbali.

Baada ya  kumaliza mapumziko hayo, jana asubuhi aliondoka kwenda Kenya ikiwa ni mara ya kwanza kufika nchini humo tangu alipostaafuu Januari 20, mwaka jana.

Rais Obama, amekuwa nchini tangu Jumapili iliyopita baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro, kisha kwenda moja kwa moja Hifadhi ya Serengeti na kukaa katika hoteli  ya kifahari ya Singita Grumet.

Awali ilifahamika kuwa Obama angewasili nchini Kenya kwa shughuli maalumu na kuonana na viongozi wakuu wa nchi hiyo, Rais Uhuru Kenyatta na makamu wake, William Ruto kabla ya kuonana na kiongozi wa upinzani, Raila Odinga.

Lakini Msemaji wa Serikali ya Tanzania, Dk. Hassan Abbas jana  aliandika kwenye ukurasa wake wa Twitter akisema: “Rais mstaafu wa Marekani, Barack Obama amehitimisha mapumziko ya siku nane pamoja na familia yake katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti nchini.”

Kabla ya kuondoka nchini, Obama aliagana na Waziri Mahiga, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira na viongozi wengine wa mkoa huo.

 

Itakumbukwa akiwa bado madarakani, Obama aliahidi atakapomaliza muda wake wa urais atahakikisha anapanda mlima Kilimanjaro kwa kuwa atakuwa raia wa kawaida, akiwa na mkewe na wanae Malia na Sasha kwa kuwa familia yake inaipenda Kenya.

- Advertisement -
Previous article
Next article

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles