30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Shibuda kuanzisha chama chake

Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda
Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda

Fredy Azzah na Esther Mbussi, Dodoma

MBUNGE wa Maswa Magharibi, John Shibuda, amesema anajipanga kuanzisha chama chake au kuhamia chama mbadala ili kuwatumikia wananchi wa Maswa kisiasa baada ya kuondoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Amesema anawaomba radhi wananchi wa jimbo lake kwa kuinadi na kuwaletea Chadema kama chama mbadala kumbe ni bati lililotoboka na kupakwa rangi na wakati huo huo wakamfanya mgambo wakati yeye alitoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) akiwa ‘Jenerali’.

Kauli hiyo ya Shibuda imekuja siku chache baada ya kutangaza kutogombea ubunge katika uchaguzi mkuu ujao kupitia Chadema.

Alisema hayo alipokuwa akizungumza na MTANZANIA katika mahojiano maalumu juzi, katika viwanja vya Bunge ambako alisema alifika kuchukua dawa kwa ajili ya mguu wake na kupata maelezo ya kinachoendelea katika kamati yake.

Pamoja na mambo mengine, Shibuda alisema kwa muda mrefu amekuwa akitukanwa huku viongozi wa chama chake wakifurahia na kumuita pandikizi la CCM, na kwamba hana ugomvi na chama hicho ila viongozi wake.

Alisema yeye kama mpangaji na Chadema, mwenye nyumba ametoa notisi ili watafute mtu wa kugombea ubunge katika Jimbo la Maswa wasije kusema amewafanyia vurugu kwenye chama chao, wakati yeye hana ugomvi na chama ila na utumishi wa viongozi.

“Kwa muda mrefu kulikuwa na minong’ono nimerudi bungeni, kila mtu Shibuda, Shibuda, sasa kidume cha mbegu ndiyo nimeingia bungeni na Wasukuma tumeaga rasmi Chadema.

“Mwaka 2015 mtaona maajabu, jana watu huko jimboni wananipigia simu wananiuliza chama gani tunaenda, vijana wanataka kuchoma bendera za Chadema nikawaambia subirini, tulieni,” alisema.

Kuhusu kutukanwa na wanachama hao, Shibuda alisema wamekuwa wakimtukana huku Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Katibu wake Mkuu Dk. Willibrod Slaa wakinyamaza kimya bila kuwaonya au kukemea hali hiyo.

“Ukiona mtoto wangu anakutukana na mimi nikanyamaza kimya maana nimemtuma au nafurahia anachokifanya, umewahi kuona gazeti la Uhuru linatukana viongozi wa CCM, kwa nini wao kila siku mnanizushia najisi.

“Nimechoka na Wasukuma wamechoka, wewe kila siku baba yako anakutukana, utasema huyu baba yangu kweli ama vipi, jiulizeni kila siku tangu nimeingia Chadema natukanwa, kipandikizi, kichomi, sijui nini.

“Nilivyokuwa namnadi Dk. Slaa waliona utamu na wakapata kura zile ambazo ndiyo zinawapa ruzuku, leo hii baniani mbaya kiatu chake dawa,” alisema.

Alipoulizwa ni kwanini asirudi CCM badala ya kuanzisha chama au kuhamia chama kingine cha upinzani, Shibuda alisema anaandaa mazingira.

“Sasa wewe mwanamke nikikupata talaka si ninatengeza mazingira ya kukukaribisha, uko katika mazingira gani ya kunivutia, wakati warembo wanazidi kuzaliwa,” alisema.

Akizungumzia kuhusu kujiunga na chama kipya cha ACT Tanzania, alisema hawezi kujiunga nacho kwa kuwa hilo ni Jeshi la Mgambo wakati yeye ni ‘Field Marshal’ wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Alisema anao uwezo wa kuanzisha chama na kikakubalika kama ilivyokubalika Chadema kabla ya kufa kibudu Maswa.

“Wewe tulia you are not professional (wewe siyo mtaaluma), kwani Chadema ilikuwepo Maswa? Nenda kaangalie, nilikinadi mimi kwa muda mfupi sana, nilipachikwa kesi ya mauaji nikashindwa kufanya kampeni kwa muda muafaka nikafanya kwa siku mbili tu, nilitengeza mtandao ukafanya kazi sasa nitashindwaje kuanzisha jeshi jipya.

“Kwa hiyo kama Mbowe na Dk. Slaa walikuwa naona hayo maneno ni matamu, basi halafu wanasema mimi ni makapi ya CCM, wananchi wangu na wapenzi wa CCM niliowashawishi wakampigia kura Dk Slaa, ni makapi ya CCM? Ndiyo shukrani, ndiyo zawadi anayowapa. Na kutokana na wao Chadema inapata ruzuku shilingi ngapi. Shukurani ya Punda ni mateke, baniani mbaya kiatu chake

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles