27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

SERIKALI YAMJIBU NAPE MRADI WA STIGGLER’S GORGE

Na Fredy Azzah, Dodoma

Serikali imemjibu Mbunge wa Mtama, Nape Nnauye (CCM), kuwa mradi wa uzalishaji umeme wa maji wa Stiggler’s George upo katika Ilani Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Majibu hayo yametolewa bungeni leo na Waziri wa Nishati, Dk. Medard Kalemani, ikiwa ni siku moja baada ya Nape kuukosoa mradi huo akisema unatekelezwa wakati haupo kwenye ilani ya chama hicho na kuachwa ule wa gesi ulio kwenye ilani hiyo.

Akijibu hoja hiyo na baadhi ya hoja zilizotolewa na wabunge waliokuwa wakichangia Hotuba ya Makadirio na Matumizi ya ofisi ya Waziri Mkuu inayotarajiwa kupitishwa na Bunge leo, Dk. Kalemani amesema ilani ya CCM imetaja vyanzo vya umeme vitakavyoendelezwa kuwa ni vya maji, gesi, upepo na makaa ya mawe.

“Haijataja mradi mmoja mmoja, imeeleza vyanzo vya umeme vitakavyoendelezwa ili tupate umeme wa uhakika mpaka tuweze kukaa hapa na kusema mwingine tuuzie majirani zetu,” amesema Dk. Kalemani.

Amesema katika kile kinachodhihirisha kuwa miradi ya gesi haijatelekezwa, mpaka sasa megawati 787 za umeme unaotumika unatokana na nishati ya gesi.

“Na hii itaendelea kwa sababu mpaka 2020 pale Kinyerezi peke yake tutakuwa na megawati 1,560 zinazotokana na gesi pekee,” amesema Dk. Kalemani.

Akitoa hoja yake bungeni jana kuhusiana na mradi huo, Nape alisema anashangaa Serikali kuweka nguvu nyingi kwenye mradi wa umeme wa Stigler’s George ambao haupo kwenye ilani ya chama hicho na kuachana na umeme wa gesi ambao waliunadi wakati wa kampeni.

“Sasa ni bahati mbaya sana kwamba humu ndani hakuna kabisa kabisa (kwenye ilani), maana yake ni kwamba hili jambo pengine limenza kuachwa sasa tuende kwenye Stiglers lakini aje, hatusaliti ilani ya Uchaguzi ya CCM?

“Lakini je hatuwasaliti wana Lindi na Mtwara ambao walitupa kura na kutuamini kwamba gesi yao na uchumi wao uko salama,” alisema Nape.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles