31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

SERIKALI KUBOMOA NYUMBA 128

bomoa

Na EMMANUEL IBRAHIM- GEITA

KAYA zaidi ya 28 zenye wakazi 128 wanaoishi Mtaa wa Kabahelele Wilaya ya Geita, juzi walitokwa na machozi mbele ya  Mkuu wa Wilaya hiyo, Herman Kapufi, baada ya kutoa amri ya kuvunja nyumba zao kwa kuwa wamevamia eneo la kituo cha afya Katoro.

Kapufi alitoa amri ya kuondoka kwa hiari ili kuokoa mali zao, baada ya Serikali kuwataka wahame kwa muda mrefu lakini wakakaidi.

Serikali imesema itabomoa nyumba zote, kuanzia Januari 11, mwaka huu.

Uamuzi wa kubomoa nyumba hizo umekuja siku chache kutokana na  tamko la Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene la kuutaka uongozi wa wilaya na mkoa kuhakikisha wanafuata agizo lililowahi kutolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, kwamba kituo cha afya Katoro ni lazima kipanuliwe ili kianze kutoa matibabu kama hospitali kutokana na mahitaji ya wananchi wengi.

Wakizungumza kwa uchungu, mmoja wa wakazi hao, Paulina Mtabazi, alisema amekuwapo ndani ya eneo hilo muda mrefu.

“Ndugu mkuu wa wilaya, nimekuja mwaka 1999, nimeishi hapa bila kuambiwa chochote, leo hii naambiwa niondoke ghafla kweli, niende wapi mimi unavyoniona ni mjane sina nguvu za kujenga, wakati mimi najenga hapa kulikuwa na jengo moja tu la kituo hicho cha afya tunaomba Serikali watuone sisi wajane,” alisema Paulina.

“Wakati nakuja kununua eneo hili nilioneshwa mipaka na mwenye eneo pamoja na viongozi kipindi hicho kulikuwa na katani, baada ya kuliona eneo tulikwenda ofisini tukawekeana mikataba, karatasi hiyo mimi ninayo wengi wetu tulikuwa hatujui zoezi hili,” alisema Paulo Magala.

Pamoja na maelezo hayo, msimamo wa mkuu wa wilaya ukawa uko pale pale  huku akipinga hoja za wananchi hao kutaka kuongezewa muda na kuwajulisha kwamba Januari 11, atasimamia kazi hiyo akiwa na polisi.

“Serikali haiwezi kuwaangalia mjenge ndani ya eneo la kituo cha afya, hakuna cha mkubwa wala mdogo, kufa ni kufa kwa hiyo nimeshawaambia hivi Jumatano asubuhi hakikisheni vitu vyenu havipo, nitakuja kusimamia zoezi la kuvunja najua mtakuwa mmeondoa vitu vyenu, mwaka 2008 mpaka leo mlikuwa mmeidharau Serikali kwamba haina lolote,” alisema.

Naye Kapufi, aliwataka wakazi hao mwenye nyaraka halali zinazomruhusu kujenga na kuishi ndani ya eneo hilo ajitokeze.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles