28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Sema wewe

MMGL0630Na Waandishi Wetu, Mwanza

SEMA wewe. Ndivyo unavyoweza kutamka baada ya maelfu ya wakazi wa Jiji la Mwanza kujitokeza kumpokea mgombea urais wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA),   Edward Lowassa jana.

Vilevile, Jeshi la polisi mkoani hapa lililazimika kupiga mabomu ya machozi kuwatawanya wafuasi wa Chadema na vyama vingine vinayounda  UKAWA ambao walikuwa wamefurika uwanja wa ndege wa Mwanza.

Mabomu hayo yalianza kupigwa ya saa 6:20  mchana.  Mabomu hayo yalipigwa baada ya wafuasi hao kutaka kuingia kwa nguvu  ndani ya uwanja wa ndege kumpokea Lowassa.

Kutokana na hali hiyo, wafuasi hao  walilazimika kusimama nje ya lango la kuingia uwanjani.

Polisi walilazimika kuchukua uamuzi huo, baada ya wafuasi hao ambao walikuwa na magari na pikipiki kutaka kuingia uwanja baada ya kuwazidi nguvu walinzi wa uwanja huo.

Msafara wa Lowassa:

Lowassa aliwasili uwanjani hapo saa 7:30 mchana na kupokewa na viongozi mbalimbali wa Ukawa.

Baada ya kusalimiana na viongozi hao msafara wa Lowassa uliondoka uwanja wa ndege wa Mwanza ukiongozwa na pikipiki.

Moja ya kituko kikubwa kilichotokea ni wakati wafuasi hao walipoamua kusafisha barabara kwa maji na kuimba wa salamu unaotumiwa na Chadema wa ‘Peoples Power’.

Hatua hiyo iliwafanya polisi kutaka kuzuia maandamano hayo lakini kila baada ya dakika wafuasi wa Chadema walizidi kuongezeka hali iliyowalazimisha  polisi kuamua kukaa kando.

Msafara huo wa Lowassa uliwasilia kwenye viwanja vya Furahisha saa 9:40 alasiri.

DIALLO, GACHUIMA

Katika hali isiyo ya kawaida jana kutwa nzima kulizagaa taarifa kuwa Mwenyekiti wa CCM  Mkoa wa Mwanza, Anthony Diallo na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC)  Wilaya ya Tarime, Christopher Gachuma, wangerejesha kadi za CCM na kujiunga na Ukawa.

Hata hivyo, viongozi hao hawakujitokeza kama ilivyokuwa imeelezwa   awali ambako umati wa wananchi ulikuwa ukisubiri kwa hamu kuwaona.

 

MBOWE NA MADAI MAPYA

Akizungumza kwenye mkutano huo, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alidai anazo taarifa  za kuwapo maofisa watatu ambao ni wataalamu wa kompyuta waliopelekwa kufanya kazi Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) katika mashine za BVR.

Alisema anao ushahidi wa kutosha na kwamba kama kuna mtu anataka ushahidi wa jambo hilo amfuate.

Mbowe alisema maofisa hao wame wamepelekwa NEC kwa masharti ya kutotambulishwa kama ni askari na wala kutokuvaa sare zao za kazi.

“Siwezi kutaja majina ya maofisa hawa sisi  tumekuja kumtambulisha mgombea wetu.  Ninaziomba mamlaka zinazohusika kuacha kuchezea nguvu ya umma, zikijaribu zitakutana nayo,” alisema.

Bila kumtaja jina, Mbowe alisema yupo mtu aliyetamka kuwa Tanzania haiwezi kuongozwa na Rais kutoka mikoa ya kaskazini na kuonya kuwa ukabila wala udini hauna nafasi kwa sasa.

“Kuna kauli iliyowahi kutolewa na kijana mmoja mpumbavu, siwezi kumtaja jina hapa kwa vile  nitakuwa namuongezea umaarufu.  Anasema nchi hii kamwe haitaweza kutawaliwa na mtu kutoka kaskazini, tuna makabila zaidi ya 150 hapa nchini… hatutamchagua mtu kwa usukuma wake wala umasai wake, tutamchagua mtu kwa vigezo,” alisema.

Mbatia kushtaki CCM

Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, alisema  anatarajia kuwafikisha baadhi ya viongozi wa CCM na jeshi la polisi katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ya Makosa ya Jinai (ICC)  Uholanzi, Novemba mwaka huu.

Alisema  kwa sasa anaorodhesha matendo yote ya jinai wanayotenda kwa ajili ya kuwafikisha huko.

Alisema NEC inapaswa kufanya kikao cha maridhiano na vyama vyote ikiwa ni pamoja na kuwazuia wakuu wa mikoa na wilaya ambao ni makada wa CCM kutoingilia shughuli za uchaguzi kwa kutoa amri kwa jeshi la polisi.

Mbatia alisema  vyama vya upinzani vinalaani mbinu chafu za kudhoofisha upinzani na kuonya kuwa kamwe hawako tayari kuona nchi inaingia katika machafuko yasiyo ya lazima.

Juma Duni Haji

Mgombea mwenza wa Ukawa, Juma Duni Haji, alisema asingeweza kuzungumza katika mkutano huo kutokana na muda finyu  na kuahidi kuwa atazungumza baada ya kuanza  kampeni na hivyo akamuachia Lowassa azungumze.

Lowassa

Akizungumza katika mkutano huo, Lowassa alisisitiza kuwa anagombea ili kuleta maendeleo.

Alisema  ataongoza kwa kuipeleka nchi katika mchakamchaka wa maendeleo na wale wasioweza kasi yake wampishe huku akionyesha masikitiko yake kwa jeshi la polisi  kuwazuia wananchi kufika katika mikutano yake kwa kuwapiga mabomu.

“Nilisema  Arusha na leo nasisitiza hapa Mwanza, tutawaburuza ICC viongozi wote ambao wanakiuka haki za binadamu.  Wanapaswa kutenda haki kwa vyama vyote na kuacha upendeleo na kuwapiga wananchi bila sababu yoyote,” alisema.

Aliwapongeza wananchi wa Mwanza na Kanda ya Ziwa kwa ujumla kwa kumpa mapokezi ya heshima na kueleza kuwa akifanikiwa kuchaguliwa atatatua matatizo ya barabara, usafiri wa meli   na kufufua viwanda   ili wananchi waweze kupata ajira.

“Najua mliahidiwa meli ziwa Victoria, machinga complex, uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwanza, pia nitaboresha reli ya kati.  Mkinichagua nitahakikisha natekeleza yote haya kwa vitendo,” alisema.

MASHA

Akizungumza katika mkutano huo, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrence Masha, alisema amerudi nyumbani akiwa na dhamira moja ya kuhakikisha taifa linakombolewa.

Alisema kwa kukishirikiana na wakazi wa Mwanza, Oktoba mwaka huu  ukombozi utakamilika.

MGEJA

Aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Hamis Mgeja, alisema mwaka 2005 aliangushwa na James Lembeli katika kura za maoni Jimbo la Kahama lakini hakufikiria kuhama chama.

“Kama nilishindwa na James Lembeli mwaka 2005 kura za maoni sikuhama vipi leo nihame kwa kuwa mwanangu ameangushwa kura za maoni?  Sikuhama kwenye nafasi ya vijana.

 

“Nataka kuwaeleza Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye na Katibu Mkuu wake, Abdulrahman Kinana wanaotuita ‘makapi’ kuwawanapaswa kutambua hayo makapi ni bora sana kwa maana yanafua umeme,” alisema.

Alisema viongozi na wanachama wa CCM kote nchini wanapaswa kujiandaa kisaikolojia kwa vile  Ukawa utaingia madarakani na kuunda serikali ya awamu ya tano.

“Ukiona nyumba inaungua usisubiri kuambiwa uondoke, niliamua kuondoka CCM kwa ridhaa yangu.  Nilipokea simu zaidi ya 800 zikipongeza kuondoka kwangu CCM lakini ni simu sita pekee zilizonipigia wakisikitika… wana CCM waliobaki waondoke,” alisema.

Machemli aibuka:

Naye aliyekuwa Mbunge wa  Ukerewe, Salvatory Machemli (Chadema) jana aliibuka na kukana kukihama chama hicho.

Wiki iliyopita  Machemli alidaiwa kuhamia Chama cha ACT Wazalendo,, lakini jana alikana akisema hana mpango huo.

“Leo hapa mnaniona sasa niwaulize hapa ni ACT Wazalendo au Ukawa.  Siwezi kuhama bado niko Chadema, siwezi kuhamia chama chochote ndiyo maana niko hapa leo hii,” alisema.

Habari imeandikwa na John Maduhu, Peter Fabian na Judith Nyange. 

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles