25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Selasini: Nitahama Chadema baada ya Bunge kuvunjwa

 RAMADHAN HASSAN -DODOMA

MBUNGE wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema), amekuwa mbunge wa pili wa chama hicho kutangaza kujiunga na Chama cha NCCR Mageuzi mara baada ya Bunge la 11 kuvunjwa Juni 30.

Pia ameomba NCCR-Mageuzi impe nafasi ya kugombea ubunge kwenye jimbo lake la Rombo katika kipindi cha 2020-2025.

Selasini ameungana na Mbunge wa Moshi Vijijini, Anthony Komu ambaye naye alitangaza kuondoka Chadema na kuhamia NCCR-Mageuzi mara baada ya Bunge kuvunjwa.

Komu pia alisema atagombea tena ubunge Jimbo la Moshi Vijijini kupitia NCCR-Mageuzi.

Selasini amekuwa Mbunge wa Rombo kwa awamu mbili (2000 – 2015 na 2015-2020) kupitia Chadema.

Pia amewahi kuwa Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni akichukua nafasi ya aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lisssu ambaye alikuwa nje ya nchi akipatiwa matibabu.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dodoma, Selasini alisema kumekuwepo na madai ya muda mrefu kwamba ana mpango wa kujiunga na CCM huku wengine wakimtabiria kustaafu siasa hali iliyosababisha kupewa majina mengi kama vile msaliti, pandikizi, mchumia tumbo na mtu wa Usalama wa Taifa.

Alisema akiwa Chadema amekutana na changamoto nyingi kutoka ngazi ya juu, hivyo kushindwa kutimiza wajibu wake.

“Nilipotumwa kazi nilifanya kazi bila kinyongo na siku zote nilipuuza maneno na mizengwe dhidi yangu kwa kuwa niliamini ni changamoto za kisiasa.

“Pamoja na hayo yote tarehe 25-04 mwaka huu siku ya Jumamosi (wiki iliyopita) nilitolewa katika grupu la Whatsapp ambalo ni nyenzo muhimu ya kazi na uongozi shirikishi ndani ya chama changu bila taarifa,” alisema Selasini.

Kutokana na hali hiyo, Selasini alisema ameamua kurudi katika chama chake cha NCCR Mageuzi kwani yeye ni miongoni mwa

 waasisi.

“Nimeamua kurudi kwenye chama ambacho nimeshiriki kukiasisi. Kama nilivyowaeleza historia yangu, mimi ni mwasisi wa mageuzi na kwa sababu hiyo nimeamua kuanzia tarehe ya leo kurudi kwenye chama changu mara nitakapomaliza shughuli zangu za Bunge.

“Na nitakiomba chama cha NCCR Mageuzi kikiridhia niweze kuendelea katika jimbo langu kupitia NCCR-Mageuzi,” alisema Selasini.

AMWELEZEA MAREHEMU MMANDA

Juzi aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Evord Mmanda alifariki katika Hospitali ya Ligula, Mtwara kutokana na maradhi ya moyo.

Mmanda ambaye kitaaluma ni mwanasheria mkongwe aliteuliwa na Rais John Magufuli kuwa DC wa Mtwara, Desemba 2016.

Selasini alisema anamfamu marehemu kama mchapa kazi mvumilivu na mpenda maendeleo kwani mwaka 1994 alifanikiwa kufanya nae kazi akiwa mwanachama wa NCCR Mageuzi akiwa Idara ya Katiba na Sheria na Haki za Binadamu katika chama hicho.

Alisema alikuwa akishirikina na Wakili Edmund Mvungi chini ya Mkuu wa Idara, Dk. Masumbuko Lamwai na Wakili msomi Ringo Tenga akiwa ni Mkuu wa Idara ya Mambo ya Nje NCCR Mageuzi.

“Mimi nikiwa ofisa tawala wa chama na sote tukiwa kwenye sekretarieti ya chama chini ya Katibu Mkuu Wakili msomi Mabere Marando, kwa kuwa kifo ni mapenzi ya mungu tunaomba Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu mahali pema peponi,” alisema Selasini.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles