30.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Samatta habari nyingine

NA BADI MCHOMOLO 

NAHODHA wa timu ya Tanzania, Taifa Stars, Mbwana Samatta, ameendelea kuwapasua vichwa mabosi wa klabu mbalimbali za Ulaya ambao wanawania saini yake katika kipindi hiki cha uhamisho wa wachezaji.

Mshambuliaji huyo ambaye kwa sasa anakipiga katika timu ya K.R.C Genk  inayoshiriki Ligi Kuu nchini Ubelgiji, anahusishwa na klabu mbalimbali, zikiwamo Aston Villa, Watford, Burnley, Leicester City na Brighton.

Hata hivyo, uongozi wa Brighton unaonekana kuja kwa kasi kushindana na klabu hizo ili kumsajili staa huyo mwenye umri wa miaka 26.

Kwa mujibu wa gazeti la The Sun la Uingereza, Brighton City, wameripotiwa kuvunja benki yao na kuweka mezani kiasi cha pauni milioni 12, ambazo ni zaidi ya shilingi bilioni 34.9 za Kitanzania kuitaka saini ya Samatta.

Kocha wa zamani wa Brighton, Chris Hughton, amedai kuwa ni shabiki namba moja wa mchezaji huyo, wakati huo kocha wa sasa wa timu hiyo Graham Petter, ameonesha kuhitaji huduma ya Samatta uwanjani.

Thamani ya mchezaji huyo imezidi kuwa kubwa baada ya kuisaidia timu yake ya Genk kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu nchini Ubelgiji.

Mbali ya kuisaidia kutwaa ubingwa, lakini mchezaji huyo, aliweza kumaliza ligi msimu huu, huku akiwa kinara wa mabao katika kikosi chake akiwa na jumla ya mabao 23.

Miongoni mwa mafanikio mengine aliyoyapata mchezaji huyo katika kikosi cha Genk ni pamoja na tuzo ya Mchezaji Bora mweye asili ya Afrika wanaocheza soka la kulipwa katika Ligi ya Ubelgiji, tuzo hiyo inajulikana kwa jina la Ebony Shoe.

Katika klabu Genk, Samatta amekuwa mchezaji wa tatu kuchukua tuzo hiyo. Miongoni mwa mastaa wakubwa waliowahi kuchukua ni pamoja na Romelu Lukaku, Michy Batshuayi na Vincent Kompany.

Nyota huyo wa zamani wa Mbagala Makert, Simba SC na TP Mazembe, alitua Genk mwanzoni mwa mwaka 2016 baada ya kufanya vizuri kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika akiwa na TP Mazembe.

Akiwa na TP Mazembe, aliweza kuibuka kuwa Mchezaji Bora wa Afrika kwa timu ambazo zinacheza Ligi ya ndani, tuzo hiyo ilitolewa na Shirikisho la Soka barani Afrika (CAF).

Kwa sasa mchezaji huyo ameungana na timu ya taifa kwa ajili kwenda kushiriki michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika, huko nchini Misri ikiwa ni mara ya kwanza kwa Tanzania kufuzu kushiriki tangu 1980.

Leo jioni Stars inatarajia kusafiri kuelekea nchini Misri ambapo itakwenda kuweka kambi kwa ajili ya michuano hiyo ambayo itaanza kutimua vumbi Juni 21.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles