24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Samatta ageuka lulu Ulaya

samatta1111111111111NA ABDUCADO EMMANUEL, DAR ES SALAAM

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Samatta, amezidi kugeuka lulu kwa timu za Ulaya baada ya matajiri wa Urusi, CSKA Moscow nao kuonyesha nia ya kumsajili katika dirisha dogo linalomalizia usajili.

Samatta aliyeondoka nchini mwishoni mwa wiki kuelekea Hispania kufanya mazungumzo na moja ya timu ya huko inayoshiriki Ligi Kuu ya Hispania ‘La Liga’, sasa amekutana na zali jingine nchini humo baada ya CSKA nayo kumfukuzia.

Mtoa habari wetu aliyekaribu na Samatta amelipasha MTANZANIA kuwa CSKA imeridhishwa na kiwango cha Samatta na inataka kumsajili kwa ajili ya kuimarisha kikosi chao kwenye mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Urusi.

“CSKA kwa sasa ipo Hispania kwa ajili ya kambi ya mazoezi kujiandaa na mzunguko wa pili wa ligi yao. Walikuwa wanamfuatilia kwa muda mrefu hivyo wanaona hivi sasa ni muda sahihi kwao wa kumsajili,” alieleza.
Mbali na timu kutoka Hispania na Urusi zinazomwania, chanzo hicho kilieleza kuwa Samatta anatakiwa na timu nyingine za Italia na Uswisi, huku timu mbili kati ya hizo nne kutoka mataifa hayo zikiwa ni washiriki wakubwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kila mwaka.

“Watanzania wasiwe na wasiwasi, taarifa njema ya Samatta inakuja muda si mrefu na itajulikana anakwenda Urusi, Hispania, Uswisi au Italia,” alieleza.

“Kwa sasa yupo Hispania na jana alitarajia kuanza mazoezi na moja ya timu hizo, watamuangalia mara ya mwisho kabla ya mazungumzo ya pande zote kuanza kisha kufanyiwa vipimo vya afya na kusajiliwa rasmi.”

CSKA iliyotolewa kwenye hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu huu ikiwa na Bayern Munich, AS Roma na Manchester City (Kundi E), kwa sasa inashika nafasi ya pili katika Ligi Kuu Urusi kwa pointi 34, huku Zenit yenye pointi 41 ikiwa kileleni.

Kama Samatta atafanikiwa kujiunga na matajiri hao wa Urusi, anaweza kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao na kuwafikia wachezaji wengine wa Afrika Mashariki kutoka Kenya, Mackdonald Mariga (wakati akiwa Inter Milan) na Victor Wanyama (wakati akiwa Celtic).

Samatta alijiunga na TP Mazembe akitokea Simba mwaka 2011, kwa sasa amebakisha mkataba wa mwaka mmoja ndani ya timu hiyo inayomilikiwa na mfanyabiashara Moise Katumbi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles