24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

SAANYA UMEIVUA NGUO FIFA

Na MARTIN  MAZUGWA-DAR ES SALAAM


martin-saanyaNDOTO ya kila mtu hapa duniani ni kufanikisha kile anachokipenda ili kuuridhisha moyo wake pamoja na watu wake wa karibu ambao wanamzunguka.

Ingawa si watu wote  wamekuwa wakifanikiwa kutimiza malengo yao waliyojiwekea katika maisha, kutokana na changamoto mbalimbali zinazowakabili.

Moja ya ndoto ya waamuzi wengi wanaochezesha ligi hapa nyumbani ni kupata beji kutoka Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), ambalo ndilo lenye dhamana ya kuusimamia mchezo wa soka.

Waamuzi wamekuwa wakijitahidi kufanya vizuri, japo waweze kufikia malengo yao hayo waliyojiwekea ili kuweza kuziridhisha nafsi zao pamoja na watu wao wa karibu.

Kati ya watu waliobahatika katika hili kwa kupata beji ya Fifa ni mwamuzi, Martin Saanya, moja ya waamuzi wenye uwezo wa kuchezesha michezo yenye presha kubwa hapa nchini na nje ya nchi.

Ni bahati iliyoje kuwa na mwamuzi kama huyu katika ligi zetu, kwani kitendo cha kuwa na mwamuzi mwenye uwezo kama wa Saanya ni jambo zuri na lenye kuvutia kwa ajili ya maendeleo ya mchezo wa soka hapa nchini.

Fifa huwa haitoi beji yao kwa kila mwamuzi ambaye anajua kuchezesha soka, bali huwa wanaangalia vitu vingi ikiwemo afya ya mwamuzi husika, uwezo wake wa kumudu presha ya mchezo pamoja na uwezo wa kujiamini.

Vigezo hivi vyote Saanya aliweza kupenya mpaka akakabidhiwa beji ya shirikisho hilo kubwa ulimwenguni, lakini hivi sasa hali ni tofauti kwa mwamuzi huyu ambaye ule uwezo wake haupo tena, jambo linaloacha maswali mengi ni kipi kilichomkumba.

Sitaki kuamini kuwa Saanya hawezi kuzitafsiri sheria 17 za mchezo wa soka, ambazo amekuwa akicheza nazo kila siku katika michezo mbalimbali aliyochezesha, ambayo imempa sifa kubwa hapa nchini na nje ya mipaka ya Tanzania.

Tayari mwamuzi huyu amekwisha ondolewa katika orodha ya waamuzi watakaochezesha Ligi Kuu ya Tanzania Bara ni aibu iliyoje kwa mwamuzi mwenye jina kubwa kama Saanya, aliyechezesha mashindano mbalimbali makubwa hapa nchini na nje ya nchi.

Hii si mara ya kwanza kwa mwamuzi huyu kufanya makosa, kwani msimu wa 2014 aliwahi kufungiwa kutokana na kushindwa kuumudu mchezo wa kati ya Yanga dhidi ya Coastal Union, uliopigwa katika uwanja wa Mkwakwani  jiji Tanga.

Kitendo hiki ni sawa na kuivua nguo FIFA, ambayo ililimwamini na kumpa heshima ya kuwa moja kati ya waamuzi bora katika ukanda huu wa Afrika mashariki na kati.

Saanya ameshindwa kuudhihirisha ubora wake, mara baada ya kuteleza kutoa maamuzi katika mchezo wa watani wa jadi kati ya Simba na Yanga ulioisha kwa sare ya kufungana bao 1-1, ambapo alikubali bao lenye utata lililofungwa na mshambuliaji Amis Tambwe.

Katika mchezo huo mwamuzi huyo pia  alimpa kadi nyekundu nahodha wa klabu ya Simba, Jonas Mkude, kwa kosa la kumsukuma, ambapo baadaye kadi hiyo iliondolewa kwa mchezaji huyo na kuonekana ilitolewa kimakosa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles