27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Rais Kenyatta amkanya mwanae kwa kuvunja amri ya kutotoka nje usiku

 NAIROBI, KENYA

RAIS wa Kenya Uhuru Kenyatta amefichua jinsi mtoto wake wa kiume alivyovunja marufuku ya kutotembea nje iliyowekwa nchini humo kuanzia saa moja jioni hadi saa kumi na moja alfajiri kuzuia kusambaa kwa virusi vya corona.

Alisema kuwa mmoja wa watoto wake wawili wa kiume, ambaye hakumtaja jina, hivi karibuni alikwenda katika sherehe usiku katika mji wa mwambao wa Kenya wa Mombasa ambao ni kitovu cha maambukizi nchini Kenya.

Mikusanyiko ya kijami hairuhusiwi katika taifa hilo lililoko Afrika Mashariki.

Serikali pia imezuia matembezi ya kuingia na kutoka katika mji mkuu, Nairobi na katika kaunti nyingine tatu za eneo la mwambao, ikiwa ni pamoja na Kaunti ya Mombasa, ambako familia yake rais pamoja na mama yake, Mama Ngina Kenyatta wanaishi kwa sasa.

Katika mahojiano na kituo cha runinga cha NTV, Rais alisema kwamba hakuna aliye juu ya hatua za kudhibiti virusi vya corona, ingawa amekuwa akikosolewa kwa kutompeleka mtoto wake katika kituo cha karantini sawa na Wakenya wengine wanaokiuka amri ya kutotoka nje wakati wa usiku.

Kenyatta alisema kuwa alimkanya kijana wake kwa kuhatarisha maisha ya bibi yake Ngina Kenyatta.

“Nikasema sawa umetoka nje na ukapata raha, lakini sasa umerudi kwa bibi yako mwenye miaka themanini na zaidi…kama chochote kitatokea kwa bibi yako kutokana na hilo ulilolifanya utaishi je …” alinukuu mazungumzo aliyofanya na mtoto wake.

MWENENDO WA COVID 19 KENYA

Waziri wa Afya nchini Kenya Mutahi Kagwe siku ya Jumatano Mei 27 alitangaza watu 123 zaidi kuambukizwa virusi vya corona.

Hiyo ndiyo idadi kubwa zaidi ya maambukizi ya corona kuwahi kutangazwa kwa siku moja nchini humo tangu ugonjwa huo uingie Kenya mwezi Machi. Hadi sasa Kenya imethibitisha watu 1,471 kuambukizwa virusi hivyo.

Wagonjwa hao wapya wanatokana na sampuli 3,077 ambazo zimepimwa hivi karibuni.

Waziri Kagwe pia alitangaza watu watatu zaidi wamefariki kutokana na corona kufikia jana na kufanya watu waliopoteza maisha kutokana na virusi hivyo nchini Kenya kufikia 55.

Kagwe alitangaza pia kuongezwa kwa muda wa udhibiti wa matembezi ya kuingia na kutoka katika maeneo ya Eastleigh jijini Nairobi na Makazi ya Old Town Mombasa

Kati ya wagonjwa hao wapya 123, jiji la Nairobi linaongoza kwa kuwa na wagonjwa 85 ikifuatiwa na 23 wa Mombasa.

Waziri Kagwe alieleza kuwa ongezeko hilo la wagonjwa linatokana na matumizi ya usafiri wa umma ambao ndio kimbilio la wengi nchini humo.

“Tumegundua kwamba watu wengi wamerejea katika namna ya usafiri wa awali, bila kujali kanuni za kujitenga na kanuni za uvaaji wa barakoa,” alisema.

Waziri Kagwe aliwataka wananchi wa Kenya kuchukua hatua stahiki za kujilinda na kuwalinda watu wengine. “Haujui unakaa karibu na nani (kwenye gari). Na kulingana na takwimu tunazozipata, nafikiri

itakuwa ni salama kudhani kuwa mtu uliyokaa ama kusimama karibu yake kuwa ana corona. Ukishaweka dhana hiyo, hautataka kuivua barakoa yako kwa kuwa utakuwa unajilinda.”

Kwa mujibu wa Kagwe, japo idadi ya maambukizi imepanda lakini kuna matumaini kwa Kenya. “…kwa ujumla wake, idadi hii ya maambukizi ni ndogo ukilinganisha na wengine na hususani idadi ya watu waliofariki kutokana na ugonjwa huu…Utaona ni idadi kubwa ya watu 123 lakini pia utaona idadi kubwa ya watu waliofanyiwa vipimo zaidi ya 3,000.”

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles