25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Rais Algeria alivyoonja joto la jiwe siku moja baada ya kutangazwa mshindi

ALGIERS, ALGERIA

RAIA wameingia mitaani katika mji mkuu wa Algeria, Algiers, baada ya matokeo ya uchaguzi wa urais.

Waandamanaji hao walikuwa wakiimba nyimbo zinazopinga kuchaguliwa kwa aliyekuwa waziri mkuu Abdelmadjid Tebboune kama rais mpya wa nchi hiyo ambaye alikuwa kiongozi mwaminifu kwa rais aliyeng’atuliwa madarakani Abdelaziz Bouteflika.

Waandamanji hao wanataka wale wote waliopo madarakani na walikuwa wanamuunga mkono Bouteflika waachie nyadhifa zao.

Siku ya kupiga kura yenyewe ilikumbwa na maandamano yaliyotaka raia kususia uchaguzi huo.

Katika matokeo hayo,  Tebboune, 74, amepata asilimia 58 ya kura zilizopigwa ambazo zinatosha kuzuia duru ya pili ya uchaguzi.

Lakini yeye na wagombea wengine walikosolewa kwa kuwa na uhusiano wa karibu na Bouteflika.

Rais Bouteflika aling’atuka madarakani baada ya kutokea kwa maandamano kote nchini humo.

Abdelmadjid Tebboune alihudumu kama waziri wa nyumba chini ya utawala wa Bouteflika pamoja na waziri mkuu kwa muda mfupi

Tebboune, mwenye umri wa miaka 74, anamrithi Abdelaziz Bouteflika, aliyelazimika kujiuzulu mwezi Aprili baada ya kuwa madarakani kwa miaka 20.

Tebboune alianza kama mfanyakazi wa umma na kupanda hadi waziri mkuu mwaka 2017 japo alihudumu kwa miezi 7 pekee baada ya kutofautiana na wafanyabiashara waliokuwa na ushawishi mkubwa.

Pia alihudumu kama waziri wa Nyumba na waziri wa Habari.

Katika kampeni yake, aliahidi kufuatilia pesa “zilizoibwa na kufichwa ulaya”.

Katika mitandao ya kijamii, Tebboune amepewa jina la utani “Mteule”.

Watumiaji wa mitandao ya kijamii wanamchukulia kuwa karibu na Mkuu wa Jeshi Jenerali Ahmed Gaid Salah.

Maafisa wa tume ya uchaguzi wamesema karibia watu milioni tisa walipiga kura katika uchaguzi uliofanyika Alhamisi huku asilimia 40 ya raia wakijitokeza.

Kwa karibia mwaka mmoja, maelfu ya raia wa Algeria wamekuwa wakiandamana kila Ijumaa katika mji mkuu na miji mingine wakipinga kufanyika kwa uchaguzi wowote chini ya utawala wa sasa.

Wanataka maafisa wote wenye kuhusishwa na rais aliyeondolewa mamlakani Bouteflika kuondolewa madarakani akiwemo rais wa sasa anayekaimu Abdelkader Bensalah na waziri mkuu Nouredine Bedoui.

“Hakuna uchaguzi utakaofanyika chini ya wahuni”, “lazima wote waondolewe”

Waandamanaji walitoa maneno hayo kila wiki wakirejea wanasiasa na wafanyabiashara wanaomzunguka rais aliyeng’atuliwa madarakani ambaye wanamchukulia kama fisadi.

Wanasema kuwa ni lazima watafutwe watu wapya kuandaa uchaguzi halisi katika nchi ambayo imekuwa rahisi kubashiri atakayekuwa rais katika uchaguzi wowote utakaoandaliwa.

Alhamisi, waandamanaji walivamia kituo kimoja cha kupiga kura mjini Algiers ambapo jaribio la maafisa wa polisi kuwafukuzwa waandamanaji lilishindwa.

Vituo vingine viwili vilivamiwa katika eneo la Kabylie, mashariki mwa mji.

Said Bouteflika, mwaka 2012, alikuwa akionekana kama nguvu kubwa nyuma ya rais

Gen Salah mkuu wa majeshi Algeria, ndiyo chanzo cha kuondoka madarakani kwa Bouteflika baada ya jeshi la Algeria ambalo lina nguvu, kumtaka Bouteflika mwenye umri wa miaka 82 kutangaza kuwa hana uwezo wa kutekeleza majukumu yake ya uongozi.

Hatua hii ya jenerali Salah ililenga kusababisha maandamano kote nchini humo dhidi ya Bouteflika ambaye alikuwa anataka kuwania tena urais kwa awamu ya tano.

Tangu Bouteflika alipong’atuliwa madarakani Aprili, wafanyabiashara mashuhuri na maofisa wa ngazi ya juu serikalini walio na uhusiano wa karibu na Bouteflika wamekuwa wakikamatwa.

Watu hao ni pamoja na Said Bouteflika aliyefungwa jela miaka 15 baada ya kupatikana na makosa ya kupanga njama dhidi ya serikali na kudharau jeshi, pamoja na wakuu wa kitengo cha ujasusi Mohamed Mediene Toufik na Athmane Bachir Tartag, na kiongozi wa chama cha mrengo wa kushoto, Louisa Hanoun.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles