Na MWANDISHI WETU
-DAR ES SALAAM
WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, amekanusha taarifa za kushiriki vikao vya kupandisha bei ya umeme.
Taarifa ya Wizara ya Nishati na Madini iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari imefafanua kwamba kikao alichokifanya Profesa Muhongo na wajumbe wa Benki ya Dunia, Septemba 28 mwaka jana, kilikuwa na mrengo wa kuboresha uendeshaji wa Shirika la Ugavi wa Umeme nchini (Tanesco) na si kupandisha bei ya umeme.
Pia taarifa hiyo ilieleza kwamba, kikao hicho kilikuwa mahususi kwa ajili ya kujadili upatikanaji wa mkopo wa Dola za Marekani milioni 200 za kufanya maboresho ya uendeshaji wa Tanesco.
Ili kuthibitisha hilo, taarifa hiyo ya Wizara ya Nishati na Madini, imetanabaisha kwamba kikao hicho kilihudhuriwa na taasisi nyingine zikiwamo Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Shirika la Madini la Taifa (Stamico), Shirika la Maendeleo la Petroli Tanzania (TPDC), Shirika la Maendeleo ya Taifa (NDC) na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura).
“Mambo yaliyojadiliwa ndani ya kikao hicho ni
upatikanaji wa umeme wa kutosha, uhakika na bei nafuu kuchochea shughuli za maendeleo ya kukuza uchumi wa nchi ikiwemo viwanda, biashara, kilimo, huduma za jamii, kuongeza ufanisi wa utendaji wa Tanesco na kupunguza deni la Tanesco.
“Hivyo katika kikao hicho, hakukuwa na makubaliano ya kupandisha bei ya umeme kama ilivyoripotiwa na gazeti hilo,” ilitanabaisha taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, habari iliyochapwa hivi karibuni na gazeti moja (si MTANZANIA) kuhusu madai ya kwamba Profesa Muhongo alishiriki kikao hicho ambacho kilikusudia kupandishwa kwa bei ya umeme haikuwa sahihi.
Taarifa hiyo ilifafanua kwamba, Wizara ya Nishati na Madini imekuwa ikifanya vikao na wadau mbalimbali wakiwemo taasisi za umma, binafsi na washirika wa maendeleo yakiwemo mashirika ya kifedha ya kimataifa kwa lengo la kuhamasisha uwekezaji katika sekta za nishati na madini nchini.
“Kuongeza ufanisi wa utendaji wa Shirika la Umeme (Tanesco), kupunguza deni la Tanesco.
Katika kulipunguza deni la Tanesco ambalo linakaribia Sh bilioni 800 (takribani Dola za Marekani milioni 363) na kuboresha shughuli za utendaji za Tanesco, Benki ya Dunia ilijadiliana na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Nishati na Madini ili kupata mkopo wa Dola za Marekani milioni 200.
“Vile vile, tunaomba kuutaarifu umma kwamba Wizara ya Nishati na Madini kwa niaba ya Serikali inafanya majadiliano na Benki ya Maendeleo ya Africa (AfDB), Umoja wa Ulaya (EU), JICA (Japan) na mashirika mengine ya fedha kwa lengo la kutafuta fedha za
kuboresha sekta ya nishati,” ilifafanua taarifa hiyo.