25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Polisi waua majambazi watano waliotaka kuiba mishahara

OSCAR ASSENGA-KOROGWE

JESHI la Polisi mkoani Tanga limeua watu watano wanaodaiwa kuwa majambazi waliotaka kupora mishahara ya wafanyakazi katika shamba la mkonge la Toronto wilayani hapa.

Tukio hilo lilitokea juzi usiku saa mbili kwenye eneo hilo ambapo majambazi hayo yaligundua siku hiyo wafanyakazi watalipwa mishahara ndipo yalipovamia na kutaka kupora fedha hizo.

Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe, alisema katika tukio hilo kulitokea majibizano ya risasi kati ya majambazi hao na askari na ndipo walipofanikiwa kuwadhibiti na kuua watano.

Alisema katika tukio hilo, Mkuu wa Upepelezi Wilaya ya Korogwe, Samson Mwandambo alipigwa risasi kifuani, lakini haikupenya kwa kuwa alikuwa amevaa nguo maalumu ya kuzuia risasi (Bullet Proof).

Bukombe alisema baada ya kupata taarifa hizo ndipo walipofuatilia na majambazi hayo yalipoona hali hiyo yalianza kurushiana risasi na askari kwa saa kadhaa.

Akielezea namna tukio hilo lilivyokuwa, kamanda huyo alisema majambazi hao walianza mapambano na askari kuanzia eneo la Mombo hadi Toronto.

 “Baada ya majibizano ya risasi na vijana wetu kwa saa kadhaa, ndipo tulipofanikiwa kuwadhibiti na kuwamaliza majambazi hayo, lakini askari wetu mmoja alipigwa risasi kifuani, kwa sababu alikuwa na ‘bullet proof’ imemsaidia hakuweza kuumia,” alisema Kamanda Bukombe.

 Alisema baada ya kumalizika kwa majibizano hayo na polisi kufanikiwa kuwaua majambazi hayo, walikuta bunduki mbili eneo la tukio aina ya shot-gun, bastola ambazo zilikuwa na risasi tano na maganda matatu ya risasi.

 Kamanda Bukombe alisema miili ya majambazi hayo imehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Korogwe Magunga kwa ajili ya taratibu nyingine.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles