27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

POLISI TANGA: TUTAWASAKA WAUZA ‘UNGA’ ANGANI, MAJINI

NA OSCAR ASSENGA- TANGA

JESHI la Polisi Mkoa wa Tanga limesema litawakamata watuhumiwa wote watakaobainika kujihusisha kusafirisha dawa za kulevya kwa njia mbalimbali ikiwamo angani, majini na bandari bubu.

Hatua hiyo inatokana na kuwapo kwa bandari bubu 45 katika mkoa huo ambazo zinadaiwa kuingiza bidhaa mbalimbali kutoka nchi za jirani.

Akizungumza jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Kamishna Mwandamizi Benedict Wakulyamba, alisema bandari bubu zilizopo wilaya za Mkinga, Pangani, Muheza na Tanga mjini zimekuwa zikitumika kufanya shughuli mbalimbali za kibiashara kwa njia haramu sambamba na kutumia vyombo ambavyo ni hatari kwa usafiri wa majini.

Kamanda Wakulyamba alisema kuwa vita ya dawa za kulevya inahitaji ushirikiano wa vyombo vya ulinzi, usalama na wananchi ili kutokomeza mtandao ambao unajihusisha na matumizi ya dawa za kulevya mkoani Tanga.

“Niseme tu ndugu zangu wanahabari nyie pia mna nafasi ya kuhakikisha suala hilo linamalizika kwa kuwafichua watumiaji na wasafirishaji, lakini pia jamii husika. Hivyo tushirikiane kuimaliza vita hii kubwa.

“Lakini sisi kama Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga, tutapambana vikali na dawa za kulevya kwa kuhakikisha tunadhibiti watu wote wanaoingiza kwa njia ya angani, majini, barabarani na njia zote ambazo zinaweza kutumika ili kutokomeza suala hili,” alisema.

Wakati huo huo, Jeshi la Polisi kupitia operesheni zake zinazoendelea mkoani hapa, limemkamata askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Koplo Rashid Mohamed mwenye namba MT 82494 akiwa na bunda 23 za mirungi.

Kamanda Wakulyamba alisema tukio hilo lilitokea Februari 9 mwaka huu na kwamba mtuhumiwa huyo alikamatwa akiwa na pikipiki.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles