25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

POGBA AMCHEFUA MOURINHO

MANCHESTER, England

IMERIPOTIWA kuwa kocha wa Manchester United, Jose Mourinho, amekasirishwa na kitendo cha Paul Pogba kuumia katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Basel ya Uswisi.

Mourinho amemtupia lawama mchezaji huyo ghali katika historia ya Man United, akimtaja kupuuzia ushauri wa madaktari juu ya tatizo lake la nyonga.

Baada ya uchunguzi wa madaktari, Mfaransa huyo aliyenunuliwa kwa kitita cha pauni milioni 89, atalazimika kukaa nje ya uwanja kwa takribani wiki sita.

Hiyo ni habari mbaya kwa Mourinho kwani amekuwa akimtegemea nyota huyo ambaye ameshapachika mabao mawili na kutoa asisti mbili katika michezo minne ya Ligi Kuu England msimu huu.

Katika mtanange huo wa hatua ya makundi uliochezwa Jumannne kwenye Uwanja wa Old Trafford, vijana wa Old Trafford waliibuka kidedea kwa ushindi wa mabao 3-0.

Itakumbukwa kuwa maumivu ya nyonga ndiyo yaliyomweka nje Pogba msimu uliopita ambapo alikosa mechi tatu.  Taarifa zimedai kwamba Pogba alitakiwa kushughulikiwa na madaktari wa timu hiyo ambao walipewa kazi ya kuhakikisha tatizo hilo linakwisha lakini mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24, amekuwa akimtumia mtaalamu wake binafsi.

Kwa kipindi hicho atakachokuwa nje akiuguza majeraha, ataukosa mchezo wa Kombe la EFL Cup dhidi ya Burton na mitanange ya Ligi Kuu dhidi ya Everton, Southampton na Crystal Palace.

Lakini pia, hatakuwa uwanjani wakati Man United watakapovaana na CSKA Moscow katika Ligi ya Mabingwa Ulaya na hata kikosi chake hicho kitakapovaana na Liverpool.

Lakini bado Mourinho hatapasua kichwa kwenye safu yake ya kiungo kutokana na uwepo wa Nemanja Matic, Ander Herrera na  Michael Carrick, huku pia akiwa na Daley Blind na Marouane Fellaini aliyeng’ara dhidi ya Basel.

Wakati huo huo, mpachikaji mabao hatari wa Man United, Zlatan Ibrahimovic, yuko mbioni kurejea mzigoni baada ya muda mrefu alioutumia kuuguza goti lake.

Pogba amemzungumzia mkongwe huyo mwenye umri wa miaka 35 akisema: “Ni mchezaji muhimu kundini na anapokuwa kwenye timu anawafanya wapinzani wahofie.”

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles